TANZANIA BORA HAITAJENGWA KWA STAILI YA BANDIKABANDUA

Ilyas, O.S @ August 2008

Katika miaka ya hivi karibuni nchi yetu imekuwa ikipita katika mitihani migumu inayotishia hatima yake kama taifa na hatima ya watanzania kwa ujumla. Mitihani ambayo kwa hali moja inatusaidia kupevuka kama taifa na kwa hali nyingine inatishia mustakabali wetu kama taifa.

Hali hii imefuata baada ya miaka kadhaa ya mtindo wa bandika bandua katika kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikumba taifa letu. Mtindo ambao kwa mantiki ya hali ilivyo sasa na dalili zinazonyesha huko tuendako, inatubidi kuachana nao haraka kabla hatujachelewa zaidi.

Changamoto tulizonazo ni lukuki ambazo ni wazi uzito wake utatuelemea. Hizi ni pamoja na tatizo la ufisadi, kuporomoka kwa maadili ya uongozi, kukua kwa hisia na kuongezeka kwa matendo ya kibaguzi miongoni mwetu, kustawi kwa matumizi ya siasa chafu, kupanuka kwa tofauti za kipato na kuongozeka kwa dalili za kuvunjika kwa muungano wetu. Kwa ujumla Tanzania ya sasa ina kila dalili mbaya ambayo hutokea katika jamii na matifa mbalimbali duniani zikiashiria kuvunjika kwa jamii hiyo ama tifa hilo.

Hata hivyo ni bahati mbaya kuwa mabadiliko yanayoendelea yamekuwa ni yale ya mtindo wa bandikabandua ambao unalenga zaidi katika kuendeleza uhalali wa tabaka tawala ambalo limejihodhisha nguvu zote za mabadiliko ya kisasa na kiuchumi badala ya kushughulikia mizizi ya changamoto hizo. Tumegubikwa na ujanjaujanja wa kushughulikia matokeo ya matatizo badala kuwa na uthubutu wa kushughulikia sababu ama mizizi ya matatizo hayo.

Hali ya ufisadi unaokomaa, kuporomoka kwa maadili ya uongozi, kukua kwa hisia na kuongezeka kwa matendo ya kibaguzi miongoni mwetu, kustawi kwa matumizi ya siasa chafu, kupanuka kwa tofauti za kipato na kuongozeka kwa dalili za kuvunjika kwa muungano wetu hayo yote ni matokeo ya matatizo na sio tatizo lenyewe.

Viongozi wetu ni lazima wakubali kuwa wakati umefika kuacha kupendelea hatua za kufunika kombe mwanawazimu apite. Viongozi wetu wanapaswa kukubali kuwa suluhu la matatizo au changamoto tunazokumbana nazo ni kuzungumzia, kukubaliana na kutekeleza makubaliano ya jinsi gani ya kuikoa Tanzania yetu na jinsi gani ya kuijenga kwa pamoja Tanzania iliyo bora kwa wote.

Ni wazi kuwa wakati umefika kwa viongozi wetu kuonyesha njia kwa watanzania kukaa kwa pamoja kujadili na kukubaliana njia mwafaka na ya muda mrefu ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazotukabili. Na viongozi wetu wakishindwa kupata uthubutu wa kuongoza katika hili basi wajue wazi kuwa si kitambo sana watanzania watajitwalia mikononi mwao jukumu hilo.

Yapo mengi ambayo watanzania tunapaswa kuwa tayari kuyaongea na kukubaliana kwa ukweli na uwazi bila ya kuogopa.

Watanzania tunahitaji kupata nafasi ya kuongelea masuala kama aina ya mfumo uchumi tupaswao kufuata, Mfumo wa kisiasa, mfumo wa muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar, Muungano wa Afrika Mashariki, sifa na maadili ya viongozi, utawala na sheria, haki na wajibu wa kijamii na jinsi gani tunaweza kuwa na mfumo wa uwezeshaji wa makundi maalumu ya kijamii bila ya kusababisha kutokuaminiana miongoni mwetu.

Tunapaswa kukaa pamoja na kuongelea kuhusu mfumo wa elimu, mahusiano kati ya vyama vya kisiasa na dola, mfumo wa uchaguzi na uwakilishi, nafasi ya vyama vya kiraia katika jamii yetu na suala zima la mila na tamaduni za kitaifa nayo ni muhimu yaka angaliwa upya kwa pamoja. Vilevile masuala ya uraia na siasa, suala heshima na maelewano ya kijamii na nafasi za viongozi wa kijamii katika uongozi wa nchi yetu.

Ni wazi kuwa hali ilivyo sasa ni ushahidi tosha kuwa wakati umefika sasa wa kuamua ni upi kati ya mfumo wa kibepari ama kijamaa tupaswao kuufuata na kwa faida ipi na njia zipi. Ni wazi kuwa bila ya uoga wowote tunapaswa kuliongelea suala la muungano ambalo kwa miaka sasa limekuwa kama donda liogopwalo kutibiwa ama hata kuguswa. Tunapaswa kulijadili sasa kuliko kuchelewa zaidi hadi kufika mahala chembe ya busara na uongozi thabiti iliyosalia, ikakosekana kabisa na kuacha chuki na dharau kuchukua mkondo kama dalili zinavyo onyesha.

Ni wazi kuwa tunapaswa kujadili suala la maadili katika jamii yetu kwa mapana yake na si hili la muono wa karibu wa siasa na biashara. Suala la maadili ni suala muhimu pia si tu kwa viongozi ambao wanapaswa kuwa kioo cha jamii lakini pia wananchi kwa ujumla. Hivi sasa jamii yetu inageuka jamii ya kichokoraa ambapo kila mtu akishindana na mwenzie kuvunja sheria za nchi na jamii kwa ujumla. Maadili sio suala la watoto na vijana wetu tu kama tulivyozoe. Ni suala la wazee, wazazi, viongozi wakuu na wadogo, matajiri na masikini, wenyeji na wageni, na watawala na watawaliwa.

Mfumo wa kisiasa nao unahitaji kufumwa upya ili kuwezesha demokrasia ya kweli kuweza kukomaa na kusaidia kujenga Tanzania yenye neema. Kamwe hili halitwezekana kama tutaendela na stili ya bandikabandua ambayo inalenga kulinda maslahi na nafsai za kundi fulani tu bila ya kujali mapungufu yanayotokana na staili hiyo ambayo yanamsabibishia mtanzania kuendelea kuishi katika maisha ya unyonge yasiyo na tija ya kimaendeleo.

Uamuzi wa kufanya mjadala huu wa kisiasa unapaswa kufikiwa sasa ili kuweza kutumia nafasi hii tuliyojikuta tunayo bila ya kuchelewa. Ni muhimu kufanikisha mjadala huo mapema ili kupelekea kutungwa kwa katiba mpya kabla ya mwaka 2010 itakayowezesha kuwa na uchaguzi ambao umefanyika chini ya mfumo mpya ulioshirikisha na kukubalika na watanzania wote. Tukawa na katiba ambayo itapata uhalali wa kila mtanzania aliye na haki ya kupiga kura.

Umuhimu wa kufanya hivyo unatokana na kuwa watanzania sasa zaidi ya wakati mwengine wowote wana shauku kubwa ya kuijenga nchi yao kwa uthabiti zaidi kama ari mpya inavyosomeka na wengi

Lakini vilevile ni muhimu kuamua sasa kwani siasa ni fani inayosifika kwa kubadili mwenendo wakati wowote ule. Kama uamuzi huo hautachukuliwa sasa na kutumia mazingira ya kisiasa na kijamii tuliyonayo sasa basi inaweza ikatokea hapo baadae hali ikawa mbaya zaidi na kulazimisha mabadiliko hayo yatokee baada ya kupitia njia mbadala ambayo itakuwa janga kubwa kwa taifa letu.

Tusingoje tufikie hali ya siasa za magomvi na chuki kama zilizowafikisha ndugu zetu wa Burundi, Sudan, Zaire (Kongo DRC), Siera Leone, Liberia walipofikia ndio tufikirie hilo. Na wala tusisubiri hali ya kutatanisha iliyojengwa katika upande mmoja wa muungano wetu yaani visiwa vya Unguja na Pemba ndipo tufikirie kufanya hilo.

Badala ya kuendelea kupoteza muda, fedha, na hata maisha ya watanzania, viongozi wetu wanaotaka kukumbukwa kwa mapendo na sio chuki dhidi yao na vizazi vyao hapo baadae, wanapaswa kuwa na uthubutu wa kushinikiza na kuanzisha mjadala wa kitaifa kuhus hatima ya nchi yetu sasa bila ya kuechelewa zaidi.

Mjadala bora na wa kujenga, daima hufanyika pale wahusika wanapokuwa katika hali ya mapendo, maelewano na heshima miongoni mwao.

Wapo wanaodhani kuwa kuanzisha mjadala kama huu ni kufungulia matatizo ambayo yanaweza kushindikana kudhibitiwa.

Wapo wanaogopa kufungulia mabadiliko kwa kuwa wanaamini hali iliyopo sasa ni hali ya kupita tu na wataweza kubadili mwelekeo na ukawa unaoridhisha kwa upande wao.
Hawa wote kwa kweli wamesahau kusoma nyakati. Mwenendo uliopo sasa hautabadilika bila ya kuwa tayari kuchukua uamuzi thabiti wa kuanzisha mjadala wa kitaifa kuhusu masuala yote muhimu yanayotusibu.

Badala ya leo kuwa na mjadala wa kuwa na KADHI, kesho mjadala wa kuhamia Dodoma, kesho kushokutwa mjadala wa URAIA, mtondogoo mjadala wa Uongozi na Biashara, ni muhimu tukawa makini zaidi na kuanzisha mjadala wa kitaifa wa pamoja ambako haya yote na mengineyo yatajadiliwa kwa mpangilio madhumubuti na utakaopunguza mzigo kwa walipa kodi wa nchi yetu.

Ni mjadala wa kitaifa tu na sio maamuzi ya bandikabandua yanayolenga kulinda mfumo fisadi tulionao ndio yataweza kujenga Tanzania iliyo na neema kwa wote kama kauli mbiu ya chama tawala CCM.

Ni mjadala wa pamoja na sio ule wa wakubwa wachache tu utawezesha kuongeza utashi wa watanzania kulitumikia taifa lao kwa nguvu na uminifu zaidi. Ni utashi binafsi wa watanzania ndio utakaorudisha nidhamu binafsi na uzalendo miongoni mwa watanzania. Na bila ya kurudisha haya tutaendelea longolongo hadi kukuche lakini Tanzania bora kamwe haitawezekana.

Tanzania bora kwa wote itajengwa kwa kushirikisha watanzania wote bila ya ubaguzi wa aina yoyote na kamwe haitajengwa kwa mtindo wa mabadiliko ya bandikabandua kama tunaoendeleza sasa.

CCM iende, Tanzania ibaki…



Na Ilyas, O.S @ July 2008

Tangia serikali ya CCM kuamua kwa shingo upande kuanzisha mfumo wa siasa za vyama vingi hapa nchini kumekuwa na taharuki kubwa ndani ya chama hiki katika kuchagua kati ya maslahi ya nchi na maslahi ya chama. Hali hii imejengwa kutokana na sababu mbalimbali ndani na nje ya chama hicho. Moja ya sababu kuu ni kubadilika kwa falsafa na mantiki ya kisiasa ya chama hicho kutoka katika kumuendeleza mtanzania hadi
kulinda na kuendeleza maslahi na nafasi ya tabaka tawala.

Ni wazi kuwa CCM ililazimika kukubali mfumo wa vyama vingi sio kwa sababu waliamini ni njia muafaka ya kulinda amani na umoja wa kitaifa. Ni wazi kuwa waiamua kufanya hivyo baada ya kung’amua kuwa bila ya kufanya hivyo wakati wakati ule basi mbeleni wangelazimika kufanya hivyo kwa matakwa na shurutisho za umma. Hali ambayo ni wazi isingewapa nafasi waliyonayo sasa ambapo bado wameweza kuhodhi nguvu za kuzuia mabadiliko ya kweli ambayo hayahakikishi usalama wa nafasi ya tabaka tawala.

Hali hii ya kubadilika kwa mantiki ya kisiasa ya CCM kutoka kujenga na kuendeleza taifa hadi kulinda nafasi ya tabaka tawala naweza kusema ndio mzizi mkuu wa matatizo lukuki tunayokumbana nayo hivi sasa. CCM wamekuwa wakijali zaidi kulinda mfumo wa kisiasa na kiuchumi tulionao ili kuepusha uwezekano wa kutokea mabadiliko ambayo yatadhoofisha nafasi ya kiutawala hata kama uhalali wao utatetereka.

Matatizo hayo ni pamoja na yale mapya ya ufisadi, uongozi mbovu, ubaguzi wa kidini, kikabila, kimapato, kirangi na hata kimaeneo na mengine ya tangia zamani kama lile la la hali na hatma ya muungano wetu. Hivi sasa wapo wanaochukulia haya kama ndio matatizo haswa na kuamua kutumia muda mwingi kufikiria, kuongea na hata kulalama mfululizo kama vile kuna uwezekano wa kuyashinda majanga haya bila ya kuyafikiria kwa mapana yake. Wapo wafanyao kosa hili bila ya kujua lakini wapo ambao wanajua wazi kuwa hali ya kufikiri hivyo ni tatizo kwani kunawezesha kuendelea kwa mfumo tulionao sasa ambao wao ni wafaidika.

Suala la ufisadi ndilo limekuwa agenda kuu ya watanzania hivi sasa kiasi cha kufikia mahala ambapo ndio imekuwa kama taswira ya CCM miongoni mwa watanzania walio wengi, wana CCM na wasio wanaCCM. Bahati mbaya agenda hii ya UFISADI badala ya kutufanya watanzania tufikirie zaidi na zaidi inaelekea kuwa imeanza kutudumaza kifikira. Agenda ya UFISADI imekuwa kama kiongeza mwendo muhimu cha kufisadisha mustakabali wa Tanzania yetu badala ya kulitetea na kulilinda taifa letu.

Wapo wengi wanaoshangaa ni jinsi gani CCM imeshindwa kulishughulikia suala hili katika njia ambayo sio tu ingeweza kuliokoa taifa letu lakini pia kuokoa nafasi ya chama hicho katika utawala wa nchi. Wengi wanaamini kuwa CCM chini ya uongozi wa Jakaya Kikwete kwa kutumia nafasi yake kama mwenyekiti wake lakini zaidi rais wa dola la Tanzania, inaweza kabisa kuchukua hatua madhubuti kuondokana na janga hili.

Hata hivyo ni wazi kuwa wanaoamini hilo wanashindwa kutambua jambo moja muhimu. Kwamba Chama Cha Mapinduzi hakijabadili tu falsafa yake kutoka katika ujamaa na kujitegemea kuelekea kusikojulikana, lakini pia kimebadili hata mantiki ya kisiasa kutoka kujenga na kuendeleza taifa hadi sasa kuwa ni kulinda nafasi ya tabaka tawala. Tabaka linalojumuisha walio wanachama na wasio wanachama wa chama hiki. CCM ya sasa sio ile ya zamani inayoamini hakuna maisha yenye umuhimu kama Tanzania. CCM ya sasa inaamini kuwa maslahi ya tabaka tawala ambalo limehodhiwa na kuneemeshwa na UFISADI yana umuhimu zaidi ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.

Ni kwa mantiki hii ndio sasa tunaona sio tu tumekuwa na ongwa la uongozi linalosababisha kushindwa kwa kuchukuliwa hatua dhidi ya wale wanaosadikiwa kuwa ni MAFISADI lakini pia sasa kuhatarisha hata muungano wetu ambao wapo walio apa kiapo cha kuulinda kwa hali yoyote ile.

Hivi karibuni kumekuwa na watu wakisema waziwazi na wengine ndani ya vikao vikuu vya CCM kuwa na tuachane na muungano. Wengi wao ni wale ambao agenda ya ufisadi imewakaba kooni hivyo wangelipenda kutumia kila njia kuondoa fokasi ya watanzania kutoka huko. Kwao wao ni bora muungano uende lakini madhambi yao yasahaulike, kwao wa ni bora Tanzania iende na CCM ibaki. Kwao wao Tanzania si chochote si lolote na CCM ndio kila kitu.

Inasikitisha na inatisha kuona kuwa hata wale walioapa mbele ya mungu na watanzania kuwa wataulinda muungano kwa nguvu zote ndio wanafikia kusema maneno kama acha muungano uende. Kwa maana nyingine wanasema acha Tanzania iende kwani ukikubali kuvunjika kwa muungano hakuna Tanzania. Inawezekana kutokana na mfumo wa muungano tulionao wapo wanaodhani kuwa tukirudisha Tanganyika bado tutabaki na Tanzania.

Inasikitisha sana kuwa watanzania tumefikishwa mahala kama hapa ambapo tupo tayari kuvunja nchi yetu ili mradi maslahi ya wachache yaendelee kulindwa. Inatisha mno kuona kuwa wafanyao haya ni wale ambao walibahatika kulelewa kwa misingi madhubuti ya muungano wetu. Yaani wale wa kizazi ambacho Mwalimu Nyerere alijitahidi kwa nguvu zake zote kukijenga katika fikira za utanzania zaidi ya yote. Hawa ndio wamekuwa wa kwanza kuusaliti muungano wetu.

Cha ajabu ni kuwa haohao wanaodiriki kusema wacha muungano uvunjike ndio kwa miaka wamekuwa mstari wa mbele kuwaita wale wanaojaribu kushauri njia muafaka za kushughulikia changamoto za muungano kuwa ni maadui wa muungano.

Katika hali kama hii ni wazi watanzania tunapaswa kujiuliza masuala kadhaa magumu yatakayotapatia majibu muhimu.

Hivi kama hawa wanafanya hivi itakuwaje kizazi chetu cha vijana wa sasa ambacho kimenyimwa malezi ya kitanzania na kukuzwa katika fikira za ubinafsi na ufisadi kitafanyaje ?

Jee, kukubali usaliti huu unaoendelea sasa wa kuthamini maslahi ya CCM zaidi ya TANZANIA yetu ndio kutatuwezesha kutatua matatizo na changamoto tulizonazo sasa?

Hivi ni kipi muhimu kati ya CCM na maslahi ya tabaka tawala ama Tanzania na maslahi ya watanzania ?

Wakati umefika wa watanzania kuamka na kuwaeleza wazi na kwa nguvu zote ndugu zetu hawa kuwa ni bora CCM iende lakini Tanzania ibaki. Uoga wao wa kuthubutu kuchukua maamuzi magumu ambayo yaweza kuhatarisha usalama wa maslahi yao lakini ukalinda na kundeleza ujenzi wa taifa letu hauna uhalali wa kuifikisha Tanzania yetu tulipoifikisha.

Wakati umefika kwa viongozi wetu ambao wangependa tuendelee kuwatofautisha wao na mafisadi mashuhuri tunaowanyoshea vidole sasa, kuthubutu kusimama kidete na kusema, ni bora CCM iende lakini Tanzania ibaki.