TULIKOTOKA: MWANZO WA SAFARI YA MWISHO YA CCM

Katika kuendeleza maoni yangu kuhusu umuhimu wa CHADEMA kushinda kwa kushindwa sasa ni vizuri kurudia makala hii hapa chini ambayo niliandika miaka sita iliyopita mara baada ya mchakato wa kupata mgombea nafasi ya Urais wa Jamhuri na Muungano kupitia tiketi ya CCM......



TULIKOTOKA: MWANZO WA SAFARI YA MWISHO YA CCM
Na Ilyas, O.S
20/05/2005

Ni ukweli usiopingika kuwa matokeo ya uchaguzi wa mgombea wa nafasi ya urais katika Chama Cha Mapinduzi yameweza kuliepusha kundi hili kisiasa katika hatari ya kugawanyika kwa kasi kama ilivyokuwa ikionekana awali.

Naongelea dhana ya kugawanyika kwa kasi tu, kwa kuwa nina uhakika kuwa mwenendo mzima wa siasa za uchaguzi huo na mambo kadhaa yaliyojitokeza katika siku za mwisho za shughuli hizo ndani ya chama hicho, zimeleta mgawanyiko mkubwa na wa hatari zaidi utakaodumu daima.

Hata kama kwa njia za ajabu mno ndugu hawa wameweza kumchagua mtu ambaye kwa maoni yao wana uhakika wa kuendelea kutawala watazania kwa miongo kadhaa ijayo.

Ni wazi kuwa CCM ya sasa si ile tena iliyokuwa ikiwavutia watu kwa utulivu wake, uongozi wa kufuata maadili ya utanzania, falsafa zake zenye kujali utu, kupinga ubaguzi na mengineyo mengi mazuri yaliyokuwa yakitofautisha chama hiki na makundi mengine ya kisiasa.

Chama cha mapinduzi kama ilivyo kwa vyama vingine vikubwa tawala barani afrika, kimepitia mabadiliko mbalimbali hadi kufikia sasa.

Mabadiliko hayo yameanzia kutoka kuwa chama cha ukombozi, kikaja kuwa chama cha kujenga utaifa na baadaye kuwa chama cha kuimarisha uchumi na kuboresha maisha ya watanzania kabla ya sasa kugeuka kuwa chama cha kuhakikisha kuendelea kubaki madarakani kwa tabaka tawala.

Mbadiliko huu umekuja kutokana na nguvu mbalimbali za kimfumo na mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi duniani ambayo yamepelekea washika dau wa chama hiki ambao mwanzo walijitahidi kukabiliana vilivyo, kuamua kufuata mkondo wa mabadiliko ili kuweza kuendelea kuongoza taifa hili.

Mfano mkubwa wa mabadiliko haya nje ya mipaka yetu ni chama cha Labour cha Uingereza kinachoongozwa na mwanasiasa “kijana” machachari Tony Blair. Chama ambacho wiki iliyopita kilipata pigo kubwa la kisiasa kwa kupoteza viti vingi katika baraza la wanaojiita wawakilishi wa makabwela.

Kama ilivyokuwa CCM, chama hiki kilianzishwa kama kundi la kutetea wafanyakazi na makabwela wa Taifa hilo la kibwanyenye.

Kama ilivyo kwa vyama vingi vya aina hii duniani, chama cha Labour kama kilivyokuwa CCM hapo awali, kilikuwa ni chama kinachoendeshwa na misingi na falsafa madhubuti za kutetea wanyonge.

Falsafa na misingi ambayo walijiwekea ili kila anayetaka kuchaguliwa kukiongoza chama hicho na hivyo kugombea nafasi ya kuongoza serikali ya Uingereza alipaswa kuonyesha wazi kuwa ni mfuasi makini na mwaminifu wa misingi hiyo kwa kauli thabiti na vitendo.

Mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi duniani yalikipelekea chama hicho kukosa mvuto wa kuaminiwa na wapiga kura wengi na hivyo kuwekwa kando katika kuingoza Uingereza kwa miaka kadhaa.

Hali hiyo iliwapelekea kundi dogo la wanasiasa vijana machachari wa chama hicho akiwemo bwana Mandelson ambaye aliwahi kuishi Musoma, Tanzania kwa miaka kadhaa akitafiti siasa ya ujama na kujitegemea na utaalamu wa kiuongozi wa baba wa Taifa, kuja na mbinu mpya walioita LABOUR MPYA.

Tofauti na Labour ya kihistoria, New Labour kama ilivyo CCM hivi sasa, ililenga matumizi ya siasa za kubabaisha zilizo tofauti na misingi na falsafa asilia ya chama hicho ili kuweza kuwalaghai wapiga kura waliokitupa, kukichagua na kukirudisha madarakani.

Kwao wao ni kuwa mara baada ya kurudi madarakani wangeweza kuzirejesha siasa makini za kihistoria za chama hicho na hivyo kuendeleza misingi na falsafa zake asilia kwa mtindo unaoendana na wakati uliopo.

Kama hapo baadae ilivyokuwa kwa upande wa wahafidhina wa chama cha Republican cha Marekani walipomchagua George W Bush kuwauzia fikira zao za kulinda nafasi ya ubabe wa marekani duniani, Mandelson na wenzake waliamua kumchagua mwanasiasa machachari aliyekuwa akikubalika wakati huo yaani Tony Blair kuongoza mpango huo.

Matokeo yake ni hali inayonekana hivi sasa huko Uingereza. Sio tu chama hicho kimegeuka kuwa cha kinyang’au zaidi kuliko chama cha mahafidhina wa kijadi cha Conservative, hivi sasa kinaelekea kaburini kwa mwendo wa kasi mno.

Kitu pekee kinachowezesha wao kuwa madarakani hadi hivi leo sio uhalali wa kidhati kutoka kwa wananchi isipokuwa propaganda za kuwapumbaza wapiga kura.

Propaganda zinazolenga kuwaweka mateka Waingereza walio wengi kwa kutumia dhana ya kuwa hakuna mwengine mwenye mvuto kama yeye anayeweza kuwalinda waingereza kwa madhila makubwa zidi kutoka kwa chama cha wahafidhina.

Ukiangalia mlolongo mzima wa historia ya chama cha Labour ni wazi kuwa kuna mambo yanayoshabihiana na hali inayojikita ndani ya chama cha mapinduzi.

Hapo zamani hata baada ya kuruhusu siasa za vyama vingi chama cha mapinduzi kilikuwa ni chama kilichokuwa kinapata wafuasi wengi kutokana na hali ya kuwa wengi wa wananchi hawa walikuwa wakijinasabisha na misingi na falsafa za chama hicho.

Hata kama wengi walikuwa wakikatishwa tamaa na matendo ya viongozi walio wengi wa chama hicho ambayo ni tofauti na sura yake asili, kuwepo kwa umakini wa kimaamuzi haswa yale makubwa kama vile mtiririko mzima wa kubadilishana madaraka kuliwapa faraja wanachi wengi waliokuwa wanaendelea kukata tamaa.

Hili na lile la kuwepo kwa baadhi ya viongozi wachache ambao tofauti na walio wengi, kauli zao na matendo yao yenye kuonyesha kuendelea kwao kuamini misingi na falsafa asilia za chama hicho, kuliwapa moyo wa matumaini watanzania walio wengi, wanachama na wasio wanachama.

Hali hii iliweza kuwazuia wanachama waaminifu wa chama hicho vijana kwa wazee, wenye sifa za umakini wa hali ya juu kutokisusa ama kutohama chama hicho kwa muda mrefu sasa.

Wengi hawa walikuwa bado wakiamini kuwa ipo siku chama hiki kitapata uongozi imara na makini utakaowezesha kurudisha chama na nchi yetu katika mstari ulionyooka na kuachana na siasa za sera za kukurupuka kwa minajili ya kuwalaghai wapiga kura tu.

Ndio maana hata hivi karibuni tulipokuwa tukishuhudia siasa chafu za kupindukia mipaka ya utanzania na ubinadamu kwa ujumla, bado walikuwepo waliukuwa wakiamini kuwa mwishoni busara za uongozi wa chama hicho zingesimama na kurekebisha mambo.

Hata hivyo hilo halikutuokea na waliukuwa wakiaminiwa kwa kazi hiyo ama walinyamaza kimya, walinyamazishwa au waliamua kukubali yaishe na kubariki siasa chafu zenye kukiuka misingi madhubuti ya chama hicho kutawala maamuzi ya vikao vyake vikuu.

Yote yanaweza kufumbiwa macho lakini kitendo cha Mwenyekiti wa chama hicho kuamua kuzuia taarifa ya siri ya sekretarieti ya maadili ya chama hicho iliyokuwa ikielezea vigezo vya kimaadili vya wagombea wote kuzungumziwa na wanakamati kuu ni kosa kubwa la kihistoria.

Maelezo kuwa wote wametoa rushwa hivyo wote sawa, kwa kweli ni upuuzi wa hali ya juu ambao kamwe hakuna aliyefikiri kuna siku Mwenyekiti wa chama hicho anaweza akaufanya.
Hata kama historia na tafiti mbalimbali zinaonyesha wazi kuwa chama hiki kimekuwa kikumbatia rushwa na kiongozi wake kuishia kutoa vitisho vya mdomo tu, lakini inapofika mkuu huyo anahalalisha uchafu huo ambao ni tofauti na nguzo kuu asili za chama hicho ati kwa kuepusha kubomoka kwa chama, ni wazi safari ya mwisho imewadia.

Lingine ni lile la kuruhusu wanakamati kuu ambao wengine ni viongozi waandamizi bila ya aibu kutumia siasa ya ubaguzi ndani ya vikao vikuu kama hivyo.

Pale machizi mbalimbali walioshindwa maisha walipokuwa wakitumia siasa haramu na chafu kama hizo kwenye vyombo mbalimbali vya habari, halali na haramu, baadhi ya watanzania makini ambao ndio walikuwa ngome ya mwisho wa chama hiki waliweza kuelewa na kuvumilia.

Lakini pale anapokuja mtu mkubwa kama waziri mwandamizi akasimama akipinga kuchaguliwa kwa fulani kwa kuwa amezaliwa akiwa na mchanganyo wa kabila au rangi fulani, na wakubwa hao wakapigia makofi, kunyamaza au Mwenyekiti akahalalisha jambo hilo kama ni demokrasia, kwa kweli hiyo ni ishara mbaya mno.

Vilevile ni dalili mbaya pale wakuu wa chama hicho na haswa wazee wenye busara waliokuwa katika makuzi ya siasa asilia za chama hicho na wengine kushiriki katika ujenzi wake wanapokuwa tayari kuweka kando maslahi ya watanzania kwa ujumla na kujali ushindi wa chama tu kama dira yao kuu ya kufanya maamuzi.

Ushindi ambao kwao wao ni muhimu tu kutokana na uhakikisho wa kuwa wao na vizazi vyao vitaendelea kuwa madarakani daima milele hata kama ishara zinaonyesha kupotea kabisa kwa utaifa wetu ambao ndio umekuwa nguzo yetu muhimu kama nchi na jamii staarabu.

Kwa ujumla ingawa wengi wanaamini kuwa chama cha mapinduzi kimeweza kuvuka mtihani mkubwa kwa ushindi, ni wazi kuwa ushindi huo unaendana na kujisimika rasmi kwa siasa mpya zisizojali misingi na falsafa asilia za chama hicho ambazo kwa kweli ndizo zimekuwa nguzo kuu za kuendelea kwa uimara wake wakati wote huu.

Siasa hizi mpya ambazo zinalenga wingi wa kura tu na sio mipango madhubuti ya muda mrefu yenye kulenga kustawisha jamii kwa mapana na marefu daima haziwezi kuifanya CCM kuendelea kuwa chama cheney mvuto asili ambo hata kama mambo hayaenda sawa wananchi wataendelea kukiamini na kikihamini.

Siasa hizi zinazofuata mbinu za soko huria ambazo zinalenga kumnadi mtu kama bidhaa nyingine sokoni zinafanya chama hicho kutegemea uhalali wa umaarufu wa mwanasiasa huyo tu na sio mapenzi na imani juu ya chama hicho.

Bahati mbaya umaarufu huu unajengwa na matarajio hewa ndani ya mioyo ya wananchi, ambayo ama kwa mapungufu ya kiutendaji ya mwanasiasa huyo au ya kimfumo ni vigumu kuyafanikisha.

Hivyo basi kukifanya chama hicho kuwa mateka wa mwanasiasa huyo na wajanja wachache waliomzunguka wanye uwezo wa kucheza na akili za wapiga kura kwa muda Fulani tu.
Hawa huwezesha hilo kwa kutumia mbinu mbalimbali za kihadaa ambazo daima huishia ama kuvuruga jamii au kuchokwa na wapiga kura.

Wapo wanaofikiri kuwa kupatikana kwa mgombea na baadaye kiongozi mwenye mvuto kama aliyechaguliwa hivi karibuni kuwa ni silaha muhimu ya kuhakikisha uimara wa chama hiki.

Mimi nasema ndio lakini ni kwa muda mfupi tu na hiyo hiyo ndiyo silaha ya kujiangamiza kwa muda mrefu.

Ni wazi ushindi uliopatikana Dodoma hivi karibuni ni mwanzo wa safari isiyo rasmi ya mwisho ya chama cha mapinduzi.

CHADEMA Ishinde kwa Kushindwa!

22 Sept 2011

Matukio ya hivi karibuni ambayo yamefanikiwa kupata nafasi ya juu katika vyombo vya habari kuhusiana na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) yamenijengea mtazamo kuwa ili CHADEMA kushinda katika safari ndefu iliyonayo kama mtawala mbadala kinapaswa kushindwa sasa.

Kitendo cha hivi karibu ambapo wafuasi na viongozi wa CHADEMA wakiwa pamoja na wabunge wawili wa chama hicho, Bwana Sylivester Kasulumbayi na Bi Susan Kiwanga kumtusi, kumkwida, kumteka na hata kumdhalilisha mkuu wa wilaya ya Igunga Bi Fatuma Kimario ni muendelezo wa dalili mbaya ya nini kinaendelea ndani ya chama hicho, ni wapi kinaelekea kama kundi la maslahi ya kisiasa na wapi kinaipeleka Tanzania yetu kama taifa.

Hata hivyo itakuwa kosa kuangalia kitendo hiki ambacho mimi nakiita kitendo cha kihuni ingawa wapo wanaothubutu kukiita kitendo cha kishujaa na ukombozi, kama tukio linalosimama pekee. Huu ni muendelezo wa mambo mengi ambayo yamekuwa yakijitokeza ndani na nje ya chama hiki kwa muda mrefu sasa ambayo yamefanya baadhi ya watu ambao hapo kabla walithubutu kuamini kuwa chama hiki kinapaswa kuwa mbadala makini wa utawala wa nchi yetu kukitazama kwa jicho la tahadhari zaidi ya matumaini.

Nadhani sihitaji kuyataja matukio hayo ambayo mengi yamekuwa yakipata nafasi ya kipekee katika vyombo vya habari na mengine yakiwa yanafunikwa haramu ipite. Hapa ningependa kulipitia tukio hili la karibuni kuangalia linaelewekaje na nini athari yake kwa CHADEMA na taifa kwa ujumla endapo wapiga kura wa Igunga ama wataweza au hawataweza kumpa ushindi mgombea wake katika uchaguzi wa tarehe 2 Oktoba 2011.

Kwa miaka kadhaa sasa na tangia kuanzishwa kwa chama hiki, kimekuwa kikiandamwa na tuhuma za ukabila na udini. Yaani chama kinachoweka mbele maslahi ya kabila, eneo na dini fulani. Kabila likiwa wachaga, eneo likiwa la ukanda wa kaskazini wa Tanzania na udini ikiwa wakristo.

Kwa kiasi fulani CHADEMA wamekuwa wakijitahidi kushughulikia tatizo hili ama kwa kukanusha ama kuchukua hatua mbalimbali za tahadhari kujivua tuhuma hizo. Hatua hizo ni pamoja na kuhakikisha mabadiliko ya mara kwa mara ya uongozi wa juu wa chama hicho ikiwemo nafasi ya Mwenyekiti.

Hatua ambayo ilikuwa kwa kiasi fulani ikionyesha dalili za mafaniko hadi mwaka 2009 zilipolazimika kutuwama ambapo kwa mara ya kwanza kilipata mwenyekiti wa kwanza wa zaidi ya muhula mmoja tofauti na ilivyokuwa hapo awali kwa Mwanzilishi Mzee Mtei (Mkristo na mchaga) na baadaye Mzee Makani (Muislamu na Msukuma).

Katika uchaguzi wa mwaka 2009, Mwenyekiti wa sasa Freeman Mbowe (Mkristo na Mchaga) kwa kutumia mbinu kadhaa alifanikiwa kuhalalishwa kuwa kiongozi wa chama hicho kwa kipindi cha pili mfululizo na hivyo kukiuka busara ya mabadiliko ya mara kwa mara ambayo yamekuwa yakihakikisha mwamko mpya(rejuvenation) wa kichama kila baada ya miaka michache.

Mabadiliko ya mara kwa mara ya uongozi wa juu yaliweza kutoa nafasi kwa chama kupanuka na kuondoa kiwingu kuwa chama hiki ni chama cha watanzania wa kabila la Uchaga na wengine ni wasindikizaji tu tofauti na wenzao wa CUF.

Uamuzi huu ulitibua nafasi ya chama hicho kuthibitishia kwa vitendo upotofu wa tuhuma za maadui zake na zaidi umma wa watanzania kuwa sio chama cha kikabila. CHADEMA ikashindwa kujiondoa katika tuhuma hizo na zaidi kujivika rasmi gamba la ukabila na udini mbele ya macho ya walio maadui na hata baadhi ya marafiki wakiwemo wanachama na wafuasi wake.

Kama vile hilo halitoshi, tukielekea katika uchaguzi wa rais na wabunge wa mwaka 2010 ambao CHADEMA ilionyesha muamko mkubwa katika medani za siasa nchini, CHADEMA ama kwa kudhamiria, kutokudhamiria au kwa kulazimika, wakafanya kosa jingine ambalo badala ya kuwanasua katika kiwingu cha ukabila na udini wakajikuta wanajisimika ndani ya wingu la Udini.

Ni ukweli ulio wazi kuwa kwa wa miaka kadhaa, wanamikakati wa CHADEMA wamekuwa wakitamani uungwaji mkono wa Kanisa la Katoliki ambao hadi miaka ya karibuni ulikuwa kama ngome muhimu ya kisiasa kwa CCM. Kwa CHADEMA kupata angalao chembe tu ya uungwaji mkono huo wa kanisa la katoliki katika chama chao ambacho wakati waislamu wamekuwa wakikiona kama chama cha waksrito zaidi, wakatoliki wamekuwa wakikiona kama chama cha Walutheri zaidi ilikuwa ni neema ya moto.

Katika uchaguzi wa mwaka 2010, kwa kiasi fulani CHADEMA ilifanikiwa kupata uungwaji mkono wa kanisa la katoliki kama mfumo imara wa kijamii na kisiasa katika nchi yetu. Hili lilikuja ama kutokana na kanisa hilo kama watanzania wengine kuchukizwa na maovu na usaliti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) au kutokana na dalili za uwezekano wa ushindi wa uhakika wa mgombea Urais wa CHADEMA ambaye ni kiongozi wa kiroho na aliyekuwa mtumishi wa ngazi za juu wa chombo nyeti cha kanisa hilo.

Kitendo cha viongozi wa kanisa la Katoliki kuanzisha na kuendeleza mpambano mkali wa majukwaani na katika alteri za kanisa kuwashutumu viongozi wa chama tawala cha CCM na serikali yake inayoongozwa na Rais na Mwenyekiti Muislamu, kabla na hata wakati wa uchaguzi huo kilijenga mtazamo wa kuwa kanisa hilo na hivyo wafuasi wake walipaswa kuiepuka CCM na wagombea wake na hivyo kuashiria kuwa CHADEMA ndio chaguo lao.

Hali hii ilileta mpasuko mkubwa wa kimitazamo katika kuelekea uchaguzi huo na hata baadhi ya wanasiasa, viongozi wa makanisa na misikiti na wapiga debe mbalimbali kuthubutu kuendeleza kampeni za udini. Kampeni zilizolenga ama katika kuhakikisha ushindi wa kutwaa nguvu za dola kwa upande wa CHADEMA na kulinda hatamu ya nguvu hizo kwa upande wa CCM.

Wakati hali hii kwa kiasi fulani iliwezesha kuongeza mafanikio ya CHADEMA katika uchaguzi wa ubunge na hata kura za urais, hali hii ilifanikiwa kusimika rasmi gamba la Udini dhidi ya CHADEMA. Kwa lunga nyingine uchaguzi wa mwaka 2010 kwa upande mmoja ulibariki CHADEMA kama chama cha ushindi kuelekea mwaka 2015 na wakati huohuo kukivika gamba la udini chama hicho ambalo ni kikwazo kwa kutimilika kwa baraka hiyo ya ushindi.

Ni katika muktadha huu wa nyota ya ubarikio wa ushindi kwa upande mmoja na gamba la dalili za laana kwa upande mwengine pamoja na matukio kadhaa tangia baada ya uchaguzi wa mwaka 2010 ndio nalazimika kujenga mtazamo kuwa CHADEMA itashinda mbele kwa kushindwa hivi sasa.

Nasema hivyo kwa kuwa naamini kama ambavyo CCM walivyokumbwa na janga la kusarandiwa, kuvamiwa na baadaye kutekwa na mafisadi, CHADEMA ya sasa sio tu imekuwa kimbilio la wajanjawajanja wanaoamini kuwa katika mtaji wa chuki kuu inayokikumba CCM miongoni mwa watanzania wanaohisi kuwa wamesalitiwa lakini pia wanaoamini kuwa ushindi wao katika duru za siasa na uchumi unahakikishwa zaidi katika CHADEMA.

CHADEMA inageuka kutoka kuwa ngome ya mapambano ya demokrasia na upingaji wa maovu dhidi ya wananchi na taifa lao na kuelekea kuwa ngome ya mafanikio ya urahisi na uhakika kisiasa na kiuchumi.

Hali hii inakifanya CHADEMA kama chama kushindwa kupata nafasi ya kujichunguza na kujitambua na pia kuwa na wanaCHADEMA wakiwemo baadhi ya viongozi wake ambao wako tayari zaidi kujidanganya na kukimbilia kukumbatia siasa hovyohovyo na za hatari kwao binafsi na kwa taifa.Siasa ambazo wanaamini ndizo zinazowavutia zaidi watanzania waliochoka na CCM na kamwe haziwezi kuwageuka.

Kitendo cha viongozi wa chama kuthubutu kumteka na kumburuza kiongozi wa serikali kinafanya wengi wajiulize maswali kama kweli chama hiki ndicho kinapaswa kuwa chama tawala mbadala. Lakini zaidi kitendo cha viongozi wa chama ambacho kinakabiliwa na tuhuma ya udini kumdhalilisha Mwanamama wa Kiislamu kwa kumvua hijabu yake kinaonyesha jinsi gani chama hicho kilivyoingiliwa na watu ambao kwa idiadi yawezekana wakawa mtaji wa kisiasa lakini kwa kimantiki ni mzigo hatari.

Mbaya zaidi badala ya kuangalia ni jinsi gani wanaweza kulisawazisha kosa hilo kubwa kisiasa, wanatokea viongozi wakuu wa chama hicho na kutoa matamsha kama vile mwanamama yule alijitakia kukumbwa na udhalilishaji huo na hata wengine kujaribu kufananisha kitendo hicho cha kihuni na juhudi za viongozi adhimu kama Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Madiba Mandela. Kama ambavyo mbunge wa CHADEMA Bwana Tundu Lissu alivyoripotiwa katika magazeti akisema.

Ni wazi kuwa wakati CHADEMA kama chama kinaonyesha kukua kwa kupata wafuasi, washabiki na hata wanachama lukuki, ukuaji huu sio ukuaji wa kuaminika.
Ni ukuaji unaotokana na ubaya wa CCM zaidi ya uzuri wa CHADEMA.

Ni ukuaji ambao unaoetegemea kufaidika na makosa ya CCM na wengine zaidi ya ukuaji wa kufaidika na mikakati madhubuti yenye kujengwa katika misingi imara itakayohimili dharuba na tufani za kisiasa.

Ni ukuaji unaopalia makaa moto wa kujimaliza kuliko ule wa kupanda mbegu za matunda ya kudumu.

Ukweli ni kuwa wakati ushindi wa CHADEMA katika uchaguzi wa Igunga utapelekea viongozi wa aina hii wa CHADEMA na wafuasi wake wengi wenye mitazamo kama ya viongozi hao kuona kuwa siasa za aina hiyo zinalipa na hazina athari kwao, kushindwa katika uchaguzi huu kwaweza kuwa nafasi adimu kwa viongozi wa chama hiki kupata ushujaa wa kukaa chini kujiangalia na kuwa na uthubutu wa kujisahihisha kabla ya ama kukutana na tufani ya kisiasa huko mbeleni au kulifikisha taifa pabaya.

Wenzao wa CCM pamoja na makosa mengi wamekuwa wakiyafanya, kimbuka kidogo cha mwaka 2010 kimewaamsha, kujiangalia na kukubali kujisahihisha kwa njia ya kujivua gamba la ufisadi. CHADEMA kwa upande wake wanapaswa kutikiswa na kaupepo cha kisiasa huko Igunga ili kukubali kujiangalia na kuanza mikakati thabiti ya kujivua magamba ya ukabila na udini ambayo ni hatari zaidi kwake na kwa jamii na taifa letu kwa ujumla zaidi ya lile la ufisadi la CCM.

Lakini zaidi kushindwa kwa CHADEMA sasa kutawezesha uongozi wake na zaidi washabiki wao kuwashinikiza kujisahihisha na kuanza kufikiri na kutenda katika taathira ya hulka ya Serikali Mbadala (Government in waiting) inayosubiri kuongoza taifa hilihili ambalo matendo yao ya sasa yanaelekea kuliharibu.

Kushindwa kwa CHADEMA sasa ni kushinda kwa CHADEMA huko mbeleni.