NINI FALSAFA YA MAPINDUZI YA CHIMWAGA 2005?

@2005..Published by Mtanzania Jumapili soon after CCM nomination process.

Baada ya miaka mingi ya Chama Cha Mapinduzi kudorora na kukosa chachandu zinazoendana na jina lake hatimaye katika hali ya kustajabisha kabisa Mapinduzi mengine ya ndani yametokea.

Ni ukweli usiofichika kuwa moja ya mbinu iliyotumika katika kuhakikisha kuwa mheshimiwa Jakaya Kikwete anashinda mchakamchaka wa kuchaguliwa kugombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi, ni kauli mbiu inayosema ARI MPYA, KASI MPYA NA NGUVU MPYA.


Lakini kubwa zaidi ni kuwa kauli mbiu hii ilikuwa na bado inaendelea kuashiria kufanyika kwa mapinduzi makubwa ndani ya CCM. Mapinduzi ambayo kwa kiasi fulani yamefanikiwa ingawa mengi bado yatakiwa kufanyika.

Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na kukua kwa mtindo wa vijana wengi wa kizazi kipya kuvaa fulana zenye picha za viongozi mbalimbali duniani ambao wamekuwa wakihusishwa na mapambano mbalimbali ya kimapinduzi.

Miongoni mwao, picha ya Hayati Ernesto Che Guevara ndio imekuwa maarufu zaidi kama ilivyo katika jamii zengine za vijana katika nchi mbalimbali duniani.

Kwa wale wasiomjua Che Guavara, huyu ni mwanamapinduzi mwenye asili ya Argentina kule Amerika ya kusini.

Mwanamapinduzi huyo amefanya mengi katika kupigania kuundwa kwa jamii isiyo na matabaka na inayoheshimu thamani ya utu wa kila mtu.

Katika jitihada zake hizo ambazo zilikuwa zikiongozwa na dira ya falsafa ya mapinduzi ya kijamaa, Che Guevara alijitolea muhanga maisha yake kwa kuwa mstari wa mbele katika mapambano ya ukombozi kuondoa tawala mbalimbali za kibepari uchwara katika pande zote za dunia.

Ni yeye ndiye akiwa begabega kwa bega na kiongozi wa CUBA, Mwanamapinduzi Fidel Castro katika mapinduzi ya CUBA. Mnamo maka 1959, Che aliongoza majeshi ya walalahoi wa nchi hiyo kuuteka mji wa Havana na kusimika utawala wa kimapinduzi wa kijamaa unaotawala hadi hivi sasa.

Ni Che ndiye aliyeamua kuacha maisha ya anasa ya kuwa waziri muhimu katika seriakali ya CUBA na kuja afrika kusaidiana na wanamapinduzi kadhaa kama Mzee Ben Bella wa FNL ya Algeria. Baadaye alijipenyeza hadi Kigoma, Tanzania alikokwenda kusaidiana na Marehemu Mzee Kabila wa DRC.

Wakati huo Mzee Kabila alikuwa akiongoza kikundi cha wanamapinduzi wanaofuata falsafa za kijamaa waliokuwa wakijaribu kurudisha madarakani masalia ya utawala wa mwanamapinduzi mwengine, Hayati Patrice Lumbumba.

Baada ya hapo, Che alienda nchi zengine zilizokuwa zikikabiliwa na unyang’au wa tawala za kibepari ambazo zilikuwa zikiongozwa na viongozi vibaraka wa Marekani, akiwa na mkoba wake uliojaa fikira za kimapinduzi.

Maisha ya mwanamapinduzi huyu yaliishia mikononi mwa mawakala wa shirika la ujasusi la marekani CIA waliokuwa wakisaidia kuulinda utawala wa kinyang’au wa RenĂ© Barrientos huko Bolivia, amerika ya kusini.

Inasemekana kuwa picha ya sura ya Che Guevara ndio picha maarufu zaidi ya binadamu yeyote kuchapwa katika vitu mbalimbali duniani.

Mimi ni moja wa vijana ambaye nimetokea kuvutiwa sana na kuvaa fulana zenye picha za wanamapinduzi hawa akiwe,o Che Guevara na kwa kweli huwa najisikia vizuri sana ninapokuwa katika vazi hilo.Lakini hilo ni tofauti na mimi ambaye nilianza kuvaa fulana zenye picha za wanamapinduzi hawa mara baada ya kusoma na kuwafahamu katika vitabu mbalimbali.

Wengi wa vijana wenzangu nchini wamekuwa wakivaa mavazi ya aina hii bila hata kujua mtu huyo wanayemshabikia ni nani na ni nini alichokuwa anakiamini na kukisimamia katika maisha yake.

Wengi hawajui kabisa ni falsafa gani ambayo Che Guevara alikuwa akiamini na jinsi gani alivyokuwa akichukia kwa ukweli kabisa madhila yaliyokuwa yakimsulubu mwanadamu yeyote yule katika pande zote za dunia.

Hali kama hii imekuwa ikionekana katika kinyang’anyiro cha na nafasi ya kugombea urais ndani na nje ya CCM.

Katika CCM kwa miaka kadhaa sasa kumekuwa na mabadiliko ya sura katika ngazi za uongozi wa chama hicho kuanzia kata hadi Taifa. Kuna wakati mabadiliko haya yalikuwa na baraka zote za viongozi wa chama hicho haswa wale wazee kama “Komredi” Kingunge Ngombale Mwiru, Mzee Rashid Kawawa, Mzee John Malecela na wengineo.

Kwao wao waliamini kwa dhati kuwa damu mpya inahitajika ili kuhakikisha kuwa chama kinaendelea kuwa na ushawishi mkubwa ndani ya jamii ya watanzania ambayo vijana ndio wawakilishi wakuu.

Bahati mbaya wazee hawa hawakuweka wazi vijana wa aina gani wanaotaka wao waaminiwe na kukabidhiwa dhamana ya kuwaongoza wenzao. Kosa ambalo sasa limewafanya wao kujikuta na mtihani mgumu wa kuamua ni nani haswa anapaswa kuaminiwa kupewa nafsi ya kuwa rais wan chi yetu kwa miaka mitano au kumi ijayo.Mtihani ambao ulihitimishwa kule Dodoma wiki iliyopita ambapo kwa kweli waliweza kuushinda kwa busara za hali ya juu.

Kwa kweli mimi kama kijana ningelipenda kuona mapinduzi haya yakitokea ndani ya chama hiki ili kukipa nguvu mpya na uhalali wa kutosha kutawala kwa ufanisi zaidi.

Lakini tatizo linakuja pale ambapo ninapoona kuwa dhana ya mapinduzi ndani ya chama ambayo hawa “vijana” wenzangu wanajaribu kuionesha inakuwa imekosa kiungo kikubwa muhimu.

Kiungo ambacho ni lazima kuwepo ili mapinduzi yeyote yale ya kisiasa au kijamii yawe yana manufaa kwa mwanachi wa kawaida aliyezingukwa na madhila yasiyo na kifani.

Kiungo hiki ni kuwepo kwa falsafa itakayoongoza mapinduzi hayo wakati wa kufanyika na baada ya kufanikiwa kubadili mfumo wa uongozi uliopo katika chama cha mapinduzi.

Siasa za kimapinduzi za mwalimu Nyerere ziliongozwa na fikira za mzee wetu huyu ambaye kwake aliheshimu kila mtu bila ya kujali kipato chake, kabila lake, rangi yake, elimu yake ama utashi wake kisiasa.

Fikira hizi zikiongozwa na kanuni binafsi za mwenendo wa kimaisha wa kiongozi huyu wetu mpendwa zenye kuendeshwa na maadili bora ya kiuongozi ndizo zilizopelekea kutangazwa kwa Azimio la Arusha.

Ni Azimio la Arusha ndilo lilionyesha wazi nafasi ya falsafa ya ujamaa na kujitegemea ambayo ndiyo iliyongoza mapinduzi ya kisiasa, kijamii na kiuchumi ndani na nje ya chama cha TANU na baadaye CCM.

Bahati mbaya tofauti na mapinduzi ya wakati huo, mapinduzi tunayoshuhudia sasa kwa kweli yamekosa kabisa kuweka wazi falsafa ambayo inaonyesha kuwa ni mapinduzi yanayolenga masilahi za mtanzania wa kawaida na sio vinginevyo.

Hivi karibuni niliweza kupata habari nyeti ambazo zilikuwa zikionyesha wazi ni wajumbe gani ndani ya halmashauri kuu ya CCM ambao wanatambulika kama wafuasi wa mapinduzi haya.

Kwa kweli ukiangalia hao wafuasi tuu ni dhahiri kuwa wengi wao si tu wamekosa utashi wa dhati wa kimapinduzi lakini zaidi hata upeo wao wa siasa za kimapinduzi ni mdogo mno.

Wengi wao katika maisha yao ya kawaida wameonyesha kuwa makuwadi wakubwa wa siasa za kibepari uchwara zenye kujali maslahi binafsi.

Wengi wao kwao ukombozi wa mtanzania wa kawaida utatokea pale tuu wao na washirika wao wachache watakapoweza kupata madaraka zaidi.

Wao ni walokole wa dhana mpya ya utajirisho inayojikita katika nchi yetu.
Dhana ambayo inaelezea kuwa dawa ya umasikini katika nchi yetu ni kuwaacha wao wachache wenye nafasi katika uwanja wa siasa na maharamia wenzao waruka kodi watajirike zaidi bila kujali maslahi ya walio wengi.

Kwa kweli dhana hii ndio inayoendesha fikira za ndugu zangu hawa waliojivika kilemba cha uwanamapinduzi. Uwanamapinduzi unaodai kulenga ukombozi wa mimi na wewe na yule.
Si bure kwao wao kuyachukulia mapinduzi yao ni ya kirika na kamwe si kifikira.

Kama ni fikira za umimi na usisi zenye kusadifiwa na falsafa ya ubinafsi ambayo sidhani kama ni falsasfa muafaka ya kuwasaidia watanzania walio wengi ambao kwao wao tatizo si sura bali mfumo mzima wa kisiasa uliowazunguka.

Tatizo la wanamapinduzi hawa wa karne mpya ni kuwa wengi wao na zaiid wale walio karibu zaidi na chaguo lao wamekosa utashi wa kujiendeleza kifikra kwa kukosa ustarabu wa kujisomea.

Wengi wao hawana tofauti na vijana wenzangu niliowaelezea hapo juu ambao wanavaa fulana na nembo zinazonyesha wanamapinduzi mbalimbali bila hata kujua nini watu hao walikuwa wakisimamia

Hawa ni wanamapinduzi wa CNN, BBC na MNET ambao kwao wao shule pekee ya kimapinduzi ni ile wanayoiona katika vyanzo hivi vya habari vikionyesha kinachoitwa “mapinduzi” mbalimbali yanayotokea katika nchi za Ulaya ya mashariki na kati.

Hawajui kwamba mapinduzi haya hayana tofauti na mapinduzi kibwanyenye yaliyotokea Uingereza, Ufaransa, Marekani katika karne kadhaa zilizopita ambayo badala ya kumkomboa mwananchi wa kawaida kutoka katika unyang’au wa kikabaila, yalisimika makabaila wapya katika sura ya ubinafsi wa kibepari.

Mbaya zaidi ni kuwa tofauti na mapinduzi hayo ya kibwanyenye ambayo yalikuwa na mwongozo wa kifalsafa uliojengwa na ujuzi wa kisayansi, mapinduzi haya ya “vijana wa CCM” yamekosa ufanisi wa kisayansi na kielimu ambo ungeweza kujenga falsafa bora na makini.

Wengi wa wahubiri wa mapinduzi haya hawana elimu wala uzoefu ya kutosha ya siasa za kidunia ambazo zingeliwawezesha kuwa na dira imara ya kulinda mapinduzi hayo mara baada ya wao kuweza kutwaa madaraka ya dola.

Na wale walioweza kubahatika kujua umuhimu wa hilo kutokana na elimu kubwa waliyonayo wengi wao wamechoka kifikira na wameamua kusalimisha silaha zao na kujitwika majoho ya ubinafsi wakisema kubali yaishe.

Wao (wasomi wachache walio katika kundi hili) wamechoka na dharuba za kimaisha wanazozipata kuotokana na misimamo yao iliyokuwa ikilenga jamii bora zaidi.

Wameamua kujiunga na timu ya ushindi na kusema kubali yaishe, bora hichi kidogo kuliko kuendelea kukosa kabisa.

Kwa kifupi wote kwa pamoja wanaamini kuwa ili kurekebisha mambo kwa haraka zaidi ni bora kuja na dhana ya mapinduzi ya kirika yenye kulenga mbadiliko wa kisura katika nyanja za utawala bila ya kujali nafasi ya fikira mbadala katika mapinduzi hayo.

Fikira ambazo zinaonyesha umakini wa kiongozi wa mapinduzi hayo ambaye daima ndiye anayetakiwa kuhodhi mawazo dira ya mapinduzi hayo na yeye mwenyewe kuweza kuyauza kwa walengwa ili kupata uhalali wao.

Inapotokea kuwa kiongozi wa mapinduzi hayo anakosa au anashindwa kuweka wazi fikira za kiuanamapinduzi zenye kujengwa na kulindwa na fasafa makini ya ukombozi wa kweli, basi hizo ni dalili mbaya za matokea ya mapinduzi haya.

Na inapotokea kuwa kiongozi wa mapinduzi hayo anakuwa amezungukwa na manyang’au wenye uchu tu wa madaraka na utajirisho wao binafsi. Waliojaa kashfa za kuwadhulumu wananchi wa kawaida basi hiyo ni dalili ya hatari kubwa zaidi.

Hata kama kiongozi huyo amekuwa akilelewa kifikira tangia ujana wake, mazingira kama yaliyomzunguka kiongozi wa mapinduzi haya yanaonyesha uwezekano tofauti kidogo.

Uwezekano ambao historia za nchi kadhaa zilizowahi kufikwa na hali hiyo zinaonyehsa jinsi gani mapinduzi kama haya yameweza kupelekea kueseka, kuabika, kunyanyasika na kuuawa kwa mamilioni ya hao waliokuwa wakidhani wanapiganiwa.

Lakini yote haya yanatokea na makosa waliyofanya wazee hawa wa CCM ambao kuanzia miaka ya mwanzo ya tisini wamekuwa wakiruhusu kila mtu kuingia katika ngazi za uongozi za chama hicho. Bila ya kujali utashi wake wa kuwahudumia wananchi na sio kujihudumia yeye binafsi.

Mbaya zaidi inakuja pale ambapo chama hiki kilipoondoa umuhimu wa elimu ya maadili na ya kifalsafa ambayo hapo mwanzo kila anayejiunga na chama hicho na haswa vijana alipaswa kipitia.

Makosa haya yote na lile la chama chenyewe kukosa mwelekeo wa kifalsafa zaidi ya falsafa ya ubinafsi ndivyo vimepelekea chama hiki kujikuta njia panda katika kuamua kama jee mapinduzi ya aina hiyo ni ya muafaka au la.

Mungu ibariki Tanzania
Mungu ibariki afrika
Mapambano daima.

No comments: