Asili za vyama vyetu na siasa za nchi yetu;



Mkataa asili hubaki kuwa mtumwa wa asili!

Vyama vya siasa kama yalivyo makundi mengine huwa vinakuwa na asili yake hata kabla ya kuwa vyama rasmi. Kuna wanaoamini kuwa hakuna dhambi ya asili ingawa usipokuwa makini asili inaweza kuwa jinamizi na hata msingi mkuu wa maendeleo yako. Mimi nakubaliana nao kwa kiasi fulani na ndio maana naamini kuwa badala ya kushindana kukana asili ya chama fulani ni vizuri na muhimu kwa maendeleo ya muda mrefu kisiasa kujitambua na kukubali asili ili kuweza kuiwekea mazingira ya kuhakisha kuwa asili hiyo inakuwa mtaji bora na sio mzigo wa miba.

Mfano ni asili ya CCM ambayo ni kikundi cha kupigania maslahi cha watu wa waliojinasibu kama waungwana wa Mzizima. Wao walikuwa wepesi kung’amua hasara ya kukataa asili yao. Hata katika enzi hizi daima inapoelezewa historia ya CCM, asili yake kama kikundi cha wachache cha maslahi ya kijamii kama ilivyokuwa katika enzi za TAA hutambuliwa na hata kuenziwa. Na asili ya CCM ina pande mbili. Pia kuna ya upande wa Zanzibar ambako nako asili ya ASP ilikuwa makundi mawili ya maslahi ya kijamii ambayo yalikuwa kundi la Wazanzibari wenye asili ya Bara yaani waafrika na wengine wenye asili ya Ushirazi.

Kwa upande mwengine wa kisiasa huko Zanzibar kulikuwa na vyama vya ZPPP ambacho hadi mwisho wake kilibaki kuwa kundi la maslahi ya kijamii katika siasa na ZNP ambacho ingawa asili yake ilikuwa ni kundi la maslahi ya kijamii kiliweza kujijenga kuwa chama cha makundi mbalimbali kabla ya kurudi nyuma kilipokaribia kuchukua madaraka kwa maslahi ya kundi la kijamii kuibuka na kuhodhi chama hicho tena na kulazimu Mapinduzi ya 1964 ambayo yalikisambaratisha hadi baadaye mabaki ya kundi hili yalipoweza kuungana na kundi maslahi la jamii nyingine na kuibuka kama CUF.

Upeo na uthubutu wa viongozi wa Tanganyika African Association kwa upande wa Tanganyika na African Association na Shirazi Association kwa upande wa Zanzibar na baadae TANU na ASP kutambua zaidi umuhimu wa kuunganisha makundi maslahi ya kijamii na kitaifa na kuunda CCM ndio moja ya misingi ya uthabiti wa CCM hadi sasa. Uthubutu wa kutambua madhara ya jinamizi la uasili hapo kabla umeweza kuwajngea msingi imara CCM na kuweza kupambana na jitihada zozote za washindani wao sasa kujaribu kutumia siasa za maslahi ya kijamii dhidi yao.

Huku bara nako kulikuwa na makundi mengine ya maslahi ya kijamii ambayo yaligeuka kuwa maslahi ya kisiasa lakini nayo yalisambaratishwa na nguvu za Mwalimu Nyerere na TANU. Kusambaratishwa kwa makundi maslahi yenye mlengo wa maslahi ya kundi fulani la kijamii zaidi ya utaifa hakukuwa na maana kuwa fikra ama mitandao ya siasa zenye mlengo wa maslahi ya makundi ya kijamii zilikwisha. Harakati za chinichini kwa chini ziliandelea na utamaduni wa maslahi siasa za maslahi ya makundi jamii kama dini, kabila ama eneo yaliendelea katika mifumo isiyo rasmi kama ilivyo mifumo ya biashara zisizo rasmi ambayo yawezekana ikawa haramu kifikra, kiitikadi ama hata kisheria lakini mifumo hiyo ikaendelea kuwepo na hata kustawi kutokana na uhalali wa kijamii.

Na hapa ndipo inapokuja asili ya CHADEMA ambayo inasemekana ilikuwa ni vuguvugu la kupigania, kulinda na kuendeleza maslahi ya kabila fulani. Yasemekana, na hili nimelifanyia uchunguzi kiasi kabla ya kulitilia maanani na natambua kuwa bado sijapata undani zaidi, asili ya CHADEMA ilikuwa ni kundi la vizito flani wanaotoka katika kabila moja ambao walianzisha kundi liloitwa ambalo lililenga kutetea maslahi ya kijamii, kiuchumi na hata kisiasa ya waanzilishi kwa kupitia kabila lao. Kundinhili lilijulikana kama Chaga Development Association. Ni wazi kama yalivyo makundi mengine ya maslahi ya kijamii kundi hili halikuwa na uhalali wa watu wote wa kabila hilo na ukweli ni kuwa lilikuwa kundi la wateule kadhaa ambao kwa mtazamo wao ilikuwa ni sawa na muhimu kwao wao kuwapigania wenzao kwa mfumo huo.

Lilipokuja vuguvugu la vyama vingi baadhi ya wateule wa kundi hili walikuwemo katika mstari wa mbele wa vuguvugu hilo ambapo baadae iliporuhusiwa kuanzishwa vyama vingi vya kisiasa, katika mijadala ya mwanzoni, mtandao wa mageuzi ya kisiasa ambao ulikuwa na watanzania wa kila aina uliafiki kuwa jina la CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO litumike kuanzisha chama cha pamoja. Kilichofuata ni sarakasi ambazo kwa mtazamo wangu ilikuwa ni makosa makubwa ambayo hadi sasa yanakisumbua chama cha CHADEMA. Wateule kadhaa ambao waliamini kuwa jina hilo halipaswi kutumiwa na kundi ambalo hawana uhakika wa kuendeleza malengo asili ya kundi lao na kudhani kuwa asili hiyo inapaswa kuenziwa katika mkakati mpya kutokana na mazingira mapya, waliwahi kwa msajili wa vyama na kusajili chama chao pekee huku wakiwatenga wenzao ambao walikuwa pamoja katika harakati za mageuzi kitu ambacho kilipekea kutumika kwa jina la NCCR badala ya CDM kama ilivyokubaliwa kwa pamoja hapo kabla.

Jinamizi la ujanja huu ndio linalokisumbua CHADEMA hadi sasa wakati kikionekana kinapata mafanikio kadhaa. Wakati vyama vingine viliweza kujitambua na kuona mbali kuhusiana na asili ya vyama vyao na kuhakikisha kuwa badala ya kuukwepa ukweli huo wanautambua na kuutumia kama somo la kisiasa, CHADEMA wao hadi sasa wameng'ana vinginevyo. Wameamua kuukana na kuukandamiza ukweli huo. Kwa mtazamo wangu hili limewapelekea kujikosesha nafasi ya kuzika jinamizi hilo kwa uwazi na udhati. Asili haipaswi kuwa kioo cha maendeleo lakini yaweza kuwa msingi mkubwa wa maendeleo. Yawe maendeleo chanya ama maendeleo hasi. Jinsi gani unaipambanua asili hiyo ndiyo inapelekea aina ya maendeleo yanayoathiriwa na asili.

Ni wazi kuwa kutokuweza kuruhusu uwazi kuhusiana na asili ya CHADEMA, iwe jina ama ajenda asilia, kunakifanya chama hicho kuwa vulnerable katika mashambulizi ya nje lakini pia mashindano ya siasa za ndani za chama pia. Kukataa asili hiyo hakuna maana hakutakuwa na wachache ambao wanaendelea kutumia asili hiyo kwa faida yao wawe maadui nje ama wa ndani au asili hiyo kutumika na wateule kadhaa kufanikisha jitihada zao za kuhodhi ushawishi wa kisiasa na kimaslahi katika maendeleo ya chama hicho na siasa za nchi. Haya hayawezi kuepukika hadi pale kutakapokuwa na utayari ya kutambua asili hiyo kwa uwazi, bila ya kujiona ni wakosa na kukubaliana kwa pamoja juu ya mikakati rasmi ya kuhakikisha asili hiyo haikwazi maendeleo ya chama hicho hasa kuhusiana na haiba yake mbele ya jamii zingine.

Hisia na wala harakati za wale wenye kuamini katika ajenda asilia hazitaisha kwa kuendeleza utaratibu wa kubadili uongozi kila baada ya kipindi cha uongozi mmoja kwisha ambao hapo kabla ulisaidia CHADEMA kuibuka kisiasa kitu ambacho hivi sasa wamekuwa wanaonekana kukidharau ama kukiogopa. Lakini ni wazi utamaduni huo kama ungeendelezwa ungeweza kupunguza mazingira ya kulistawisha suala la hisia za ukabila ama maslahi asilia. Naamini kuwa kwa faida ya CHADEMA lakini zaidi kwa faida ya nchi yetu na kutuepusha kubaya zaidi tunakoelekea, muungano wa CHADEMA na CUF ni muhimu sana ingawa wengi wanaona hilo kama ni ndoto tu kutokana na kutambua nguvu za maslahi ya makundi ya kijamii katika vyama vyote hivyo ingawa wasengependa suala hilo kuongelewa kwa uwazi.

Ieleweke kuwa siamini kuwa hadi sasa CHADEMA ni chama cha ukabila. Ni wazi agenda rasmi ya CHADEMA kama chama cha siasa chenye uhitaji wa kukubalika kitaifa haiwezi kuwa maslahi ya ukabila. Lakini hiyo haiondoi ukweli kuwa nguvu za maslahi ya kijamii ambayo ndio yalikuwa ajenda asilia zinaweza kuendelea kuathiri maendeleo ya chama hicho. Hiyo inaweza kutokana na kuendelea kwa fikra asili miongoni mwa baadhi ya wateulena ambazo zikaendelea kuwa na nguvu kiasi fulani ama mtazamo wa watu dhidi ya chama hicho kutokana na asili yake hiyo ambayo imeweza kuathiri haiba ya chama hicho hasa kutokana na kushindwa kulikabili zimwi la uasili kwa uwazi na upana wake.

Chukulia mfano wa suala la uongozi wa chama hicho. Angalia zile harakati za kumrithi Mzee Mtei ambapo kulikuwa na jitihada nyingi za kumrithisha Mzee Ndesamburo ambaye naye ni mmoja wa wa wa kabila hilo na alikuwemo katika mkakati asili. Kilichotokea ni mgawanyiko mkubwa wa chama baada ya kushinda Mzee Makani ambaye kwa wenye kuendeleza fikra za agenda asilia walimuona kama wakuja na kufikia kukizira chama hadi pale kiliporudi mikononi mwa mwenzao ambaye anaweza kuaminika, kuhalisia ama kihisia, kulinda nafasi na maslahi ya agenda asilia.

Hili pia limethibitishwa na yaliyowatokea kina Mzee Mchata, Mzee Ngululupi, Kaburu, Wangwe, Zitto na wengineo wengi walionekana kutishia nafasi ya ajenda asili. Na haya yanaendelea hadi sasa katika harakati za M4C ambazo ingawa zimewezesha kukitanua chama kwa maana ya idadi ya wanaojiunga lakini kinaendelea kukigawanya chama hicho katika siasa za ndani. Ni wazi kuwa kushindwa kulikabili janga la uasili kwa uwazi, udhati na uthabiti kunaendelea kuwa kikwazo cha kuondokana na haiba ya maslahi jamii hata kama kuna kutambua kuwa suala hilo linaathari yake kwa mipango ya kisiasa ya chama hicho. Bila ya kulikabili jinamizi hili kwa uwazi na ushiriki mpana litaendea kuathiri chama na siasa za nchi hata pale ambapo chama hiki kitakapoweza kufanikia kukwapua madaraka kutoka kwa washindani wao.

Kuhusiana na kukubalika kwa CHADEMA katika pande mbalimbali za nchi ama makundi mbalimbali ya kijamii hilo halina maana kuwa athari za uasili hazipo ama hakuna wanaondeleza siasa za agenda asilia kichinichini. Lakini pia unaposema kukubalika kwa maana ya kuwa chama hicho kimeweza kupata viti vya kisiasa bila ya kuangalia factor zingine za kisiasa katika maeneo hayo au idadi ya kukubalika kwa muktadha wa ujumla wa kura zote za eneo tajwa, nadhani kaka unakosea. Ni wazi kuwa kupigiwa kura hakuna maana a kukubalika pekee bali kunajengwa na sababu nyingi na hivyo kutoa maana nyingi. Kwa mfano, ni wazi kuwa jimbo la Ausha na yale ya Mwanza yalienda CHADEMA sio kwa sababu ya kukubalika kwa chama ama mgombea bali ni ushindani wa kisiasa na kimaslahi ndani ya CCM. Tukumbuke, hisia za kisiasa zinaweza kuwa na mahusiano ya hisia mbalimbali za kijamii, kisiasa na hata kiuchumi hivyo haziwezi kutafsiriwa kwa muktadha mmoja tu.

Ukweli ni kuwa hizi siasa za maslahi ya makundi jamii zipo hata CCM. Hivi sasa makundi ya kikabila, kimikoa, kidini, kimaeneo, kikanda yanaendelea kushamiri ndani ya CCM. Tofauti ya CCM na vyama vingine ni kuwa kwa CCM jinamizi hili lilitambuliwa na kushughulikiwa mapema hivyo kujenga mfumo na utamaduni wa kisiasa ambao hakuna kundi lolote linaloweza kuhodhi nafasi ama kwa kiasi kikubwa au kwa muda mrefu na hivyo kuweza kuhakikisha kuwa hakuna kundi linalojiona wakuja ama wateule na ushindani wao unakuwa maintained katika muktadha huo.

Kukimbilia kupiga kelele za ukabila kila wanapotokea wenye uthubutu wa kuliweka suala hilo wazi, ama kwa faida ya makundi mengine ama kwa faida ya siasa makini hakusaidii hatma ya chama na wala hatma ya siasa zetu. Bila ya kutambua umuhimu wa mjadala wa wazi wa mambo mbalimbali ya kweli ama ya hisia hakuna kikundi cha siasa ambacho kinaweza kufanikiwa katika mazinira ya jamii, utaifa na siasa za Tanzania. CHADEMA na vyama vingine kama CUF wanapaswa kuondokana na utumwa wa kukataa asili na ndipo mwatakapoweza kuthubutu kuchukua hatua za dhati na madhubuti ya kuondokana na jinamizi la asili! Jinamizi hili litaendelea kusinya na hata kudumaza maendeleo ya kisiasa hadi pale watakapokuwa tayari kulizika rasmi kwa uwazi na ushirikishi wa dhati wa makundi mengine kijamii.

Kuendelea kukandamiza mijadala ya suala hili kunaendeleza hisia za kutokuamini haiba na malengo hasa ya chama hicho na pia kunatoa mwanya kwa baadhi ya wanaojiona ni masalia ya wateule wa agenda asilia kuendelea kuamini katika matumizi ya uasili huo kwa faida yao na wakati mwengine hata chama chao lakini kwa upande mwengine kuendelea kukigharimu chama katika muktadha wa maslahi ya muda mrefu. Hili nalo lipo kwa upande wa CUF ambayo historia imeshawaonyesha jinsi gani jinamizi hilo linavyweza kuwa na faida ya muda mfupi lakini hasara ya muda mrefu na bila ya kusahau MTIKILA na kundi lake la siasa za wazawa dhidi ya wakuja zilipomfikisha.

No comments: