KIKWETE CHAGUA MAARUFU, SALIM CHAGUO MAKINI. (Sehemu ya kwanza)

Published by Mtanzania Jumapili@ 2005

Hata kama kuna wengi watakaokasirika, ni ukweli ulio wazi kuwa uteuzi wa mgombea wa Urais wa Tanzania kupitia chama cha CCM utakaofanyika tarahe Mosi mwezi Mei 2005 kule DODOMA, ndio utakao amua kuwa harakati za kumtafuta rais wa Tanzania kwa miaka mitano au kumi ijayo zimekwisha au ndio kwanza zinaanza.

Nasema hivi kwa kuwa ni wazi kati ya wagombea wote waliojitokeza kuna wagombea wawili au watatu ambao wakipitishwa, sio tu watatoa nafasi kwa vyama mbalimbali vya upinzani ambavyo bado havijaweza kujiuza vyema kwa watanzania kujitutumua kisiasa na kutoa upinzani mkali kwa baba wa dola, yaani CCM.

Lakini vilevile kuna wagombea wengine wawili ambao kwa kweli CCM ikimpitisha mmoja wapo na mwingine kutopiga kelele za mizengwe, basi ushindi wa kishindo unakuwa tayari umeshajikita kwa ndugu zetu wa hawa, yaani CCM.

Wawili hao si wengine bali ni Mtanzania mmoja maarufu hapa nchini na pande zote za dunia, Dr Salim Ahmed Salim na mwengine maarufu sana hapa nchini na maeneo mbalimbali katika maziwa makuu ya afrika, Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete.

Ni ukweli usio fichika kuwa Ndugu Kikwete ni chaguo maarufu kabisa kupita wote waliojitokeza kuwania nafasi hii kupitia CCM, akifuatiwa kwa mbali ingawa hali inaonekana kubadilika kwa kasi mno, na Dr Salim Ahmed Salim.

Sababu za umaarufu huu ambao kwa kweli ni muhimu kwa taifa linalozidi kupoteza mwelekeo kila kukicha, ni nyingi na mimi nitajitahidi kuzitoa kwa kadri ya niwezavyo bila ya unafiki.

Ndugu Kikwete ambaye ni mwanasisa mkongwe ndani ya CCM tangia ujana wake, chini ya usimamizi wa Mwalimu Nyerere ambaye yeye anasahibiana naye kwa undugu wa kiapo, kwa wanaokumbuka mchango wa Sheikh Bharamiya wa kule Bagamoyo ambaye anasahibiana naye, kikwete ameweza kujitokeza kama mwnasiasa kijana tangia pale alipogombea na kushindwa nafasi hiyo mwaka 1995 akiwa na umri wa miaka 45.

Hivi sasa ndugu huyu anakaribia miaka 55, lakini kutokana na kujitambulisha zaidi na vijana ambao ndio wengi wanaonekana kumzunguka, na hulka yake ya uhalisia “simplicity”, ndugu huyu ameweza kujitengenezea mhimili wa kisiasa katika jukwaa la vijana ambao ama kwa bahati au kwa makusudi wameweza kupenyeza ngome za CCM kwa wingi kuanzia mwaka 1998 na kuendelea.

Wako wanaohoji kuwa yeye si kijana lakini ningependa kuwakumbusha kuwa ujana unaozungumziwa hapa si umri bali ni fikra, ambazo vijana walio wengi ambao ndio wamiliki halali wa taifa hili wanaamini kuwa Ndugu Kikwete pekee ndiye anayewakilisha ndoto zao za kuondokana na ufedhuli wa kimaisha unaotugubika.

Kingine ambacho Ndugu Kikwete ameweza kukiwakilisha kwa jamii, ni dhana ya uasi wa ndani UASI WA NDANI ya mfumo wa kuhafidhina wenye kuendeshwa na falsafa ya rushwa iliyokithiri ndani ya Chama kinachojiita cha Mapinduzi.

Ukiondoa karibia wote wanagombea nafasi hiyo ndani ya CCM, Ndugu Kikwete ndiye pekee mwenye kuonyesha kuwa ni kweli mwakilishi wa wakulima na wafanyakazi wa tabaka la kati na la chini kutokana na haiba yake ya uhalisia. Ndugu huyu ambaye ama kwa uthabiti wa kimaadili au mahesabu ya kisiasa, pamoja na mambo mengine ameweza kukataa “kuzawadiwa” nyumba zilizojengwa kwa jasho na damu za watanzania, kitu ambacho kinawapa matumaini vijana na wazee wengi kuwa ataweza kupambana na rushwa na hata kusafisha uozo huo ndani ya CCM na tabaka tawala kwa ujumla.

Sifa nyingine aliyonayo Ndugu Kikwete ni suala la mvuto. Hili kwa kweli ni silaha kubwa ambayo hata wenzanke wakimdhihaki vipi, kamwe hawataweza kumuangusha. Suala la sura ya mvuto ni muhimu sana kwa jamii iliyokata tama kama Tanzania.

Sio kwamba inampaa wapenzi wengi kisiasa hasa wale wa jinsia tofauti naye ambao ndio wenye kura nyingi zisizotetereka kirahisi ndani na nje ya CCM, sura na haiba ya mvuto ni silaha muhimu kwa kuongoza katika mwenendo wa siasa za kimaarufu “popular politics” ambazo wengi tunadhani zinahitajika ili kusafisha uozo wa kisiasa tulionao.

Uozo ambao umejengwa na kulindwa na baadhi ya wagombea pinzani wa ndugu huyu ambao watanzania wengi hasa vijana wangependa kuona wanatoka katika medani za kisiasa.

Sifa za Dr Salim duniani nadhani wote twazijua, sio tu kutokana na majukumu mbalimbali ya kitaifa na kimataifa ambayo aliwahi na bado amekabidhiwa na wanadunia, lakini pia haiba yake ya unadhifu wa kisiasa ya mfano wa Mwalimu wake kipenzi, hayati Mwalimu Nyerere ambayo kwa sasa imekuwa ni fimbo muhimu katika jaribio lake la kuomba dhamana ya kuwaongoza watanzania moja kwa moja kama Rais wa nchi yetu.

Mengi yamesemwa kuhusu Dr Salim lakini mimi ningependa kwa kutumia kautaalamu kangu kadogo cha uchambuzi wa siasa wanachonipatia wasomi wetu pale mlimani kwa miaka kadhaa hivi sasa, kuongezea yale machache ambayo nadhani hayasemwi au hayajasemwa bado na vyopmbo vyetu vya habari.

Kutokana na upeo wa juu alionao ndugu huyu kuhusiana na mambo ya siasa za kidunia, Wengi na hata kutoka vyama pinzani na CCM wanaona Dr Salim anaweza kuwa ndio tunu ya nchi yetu kutupeleka kwenye Demokrasia ya kweli na si kwa maneno tu bali kwa vitendo.

Kwa wengi wanovutiwa naye, hilo kwake hakuna mjadala kwani ingawa wengi hubadilika na nguvu za madaraka, kwake yeye kama aliyewahi kuwa kiongozi wa mapambano dhidi ya unyonge, ukoloni na ubaguzi wa aina yeyote popote pale duniani pamoja na kuwa mpiga mbiu mkuu wa utawala wa demokrasia ya kweli barani Afrika, kufanya tofauti utakuwa ni unafiki ambao hata mtu asiye na haiba ya aibu hataweza kufanya hilo.

Lengine ni kuwa uhusiano wake wa karibu na Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Nyerere ambye ndiye amekuwa dira yake kisisasa. Uhusiano huo na mwalimu pamoja na wale watukufu wengine wa zamani (Disgruntled old guards) ambao walilitumikia taifa kwa adabu na heshima ya juu kwa wananchi.

Hawa ni kama wazee wetu akina Judge Warioba, Mzee Ibrahim Kaduma na wengineo wachache lakini washupavu ambao hadi sasa wanajaribu kuwa nguzo na dira ya dhana ya utawala wa kamaadili ambao kwa kweli umemong’onyoka mno kama sio kuisha kabisa. Hawa wameweza kumpa Dr Salim imani ya kuwa ataweza kurudisha utawala wa nidhamu ya kimaadili nchini.

Katika safari yake kuelekea uchaguzi, Dr Salim ameweza kuonyesha kuwa mbali na kusimamia ujenzi wa uchumi imara lakini anaweza kurudisha dhana ya maadili ambayo si tu tunaihitaji kwa kulinda haka kaamani ketu kwa kulinda utu wa kila mtanzania bila ya kujali nafasi yake kiuchumi, bali pia kutupunguzi janga la ukimwi ambalo kwetu sisi ni adui kama ilivyo ugaidi wa kidini kwa Taifa la Marekani hivi sasa.

Kingine ambacho haka kaupeo kangu ka kuchambua masuala ya siasa kameweza kunionyesha ni kwa msomi kama Dr Salim ambaye sio tu wa darasani bali hata katika kufikia maamuzi yake, ni dhahiri atweza kusimamia kuona kuwa thamani ya usomi makini na wasomi wetu itarudishwa.

Katika duru ya wasomi, ingawa si wote, wengi hata wale wanaompinga kwa sababu zingine wanaamini kuwa Dr Salim ataweza kutumia vyema nafasi ya kutuongoza kunusuru hali ya mbambo katika madhabahu zetu za kisomi na elimu, ambazo sio tu hali inatisha bali pia ni hatari kubwa kwa taifa letu hasa katika dunia hii ya ushindani usiokuwa na huruma wala haiba.

Bila ya kuwa ni kiongozi anayethamini hali na mawazo wa wasomi, kutambua umuhimu wa ELIMU BORA na sio BORA ELIMU, anayejiongoza kisiasa na kuwaongoza wananchi wake kwa lugha na mtindo wa kisomi, ni wazi hata tukiletewa malaika, safari ya tunapoelekea kusikojulikana itakuwa ya mwendo kasi na wa hatari mno.

Lingine ambalo kwa kweli si ajabu kuona watanzania wengi wa kizazi chetu hawakioni ni kuwa watanzania kama washika dau wakuu wa dunia ya tatu, au kwa kifupi masikini wa dunia, hivi sasa tunakabiliwa na zoezi kubwa la kupambana kuweza kupata mfumo wa siasa za kimataifa ambo utatambua na kutetea zaidi maisha yetu kiuchumi na kijamii kwa miaka mingi ijayo.

Hili ni suala la marekebisho mbalimbali katika mfumo wa umoja wa mataifa (UN) ambao kutokana na mchango wa Dr Salim na viongozi wenzake wengi wapatao kumi na tano pamoja na wasomi wetu kama Prof Mwesiga Baregu na Prof Haroub Othman, kuanzia mwezi September 2005 kule New York, Marekani na kwengine pote duniani, majadiliano makali yataendelea kujaribu kubadili mfumo wa kimataifa.

Mfumo ambao kwa miaka mingi umekuwa ukiwapendelea mno mataifa makubwa na tajiri dunia na kukandamiza ndoto zetu za kupata ahuani ya kweli ya kimaisha. Kwa kweli kama hatutakuwa na kiongozi shupavu, makini, msomi, mwenye kuheshimika katika medani za kimataifa na mjuzi wa hali ya juu wa masuala haya, Tanzania ambayo ina jukumu la kuongoza sauti ya wanyonge kupitia nafasi yetu katika baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kama mwanachama wa muda kwa miaka miwili kuanzia mwezi January mwaka huu, ni dhahiri mpambano huu tunaweza tukaupoteza hivyo tukawa tumejisaliti na kuwasaliti mabilioni ya wanadunia masikini na wanyonge wanaotegemea sauti yetu huko.

Nasisitiza hili kwa sababu najua wazi kuwa bila ya kubadili mfumo wa siasa wa kimataifa, hata kama utaletewa malaika wa juu kabisa, kamwe mbio zetu zitaishia ukingoni na kuendelea na siasa za longolongo, kama wanavyosema vijana wa mjini.

Ukiangalia hizo baadhi ya sifa za wagombea hawa wawili wa CCM hapo juu na nyingine nyingi zilisosemwa na zinazosemwa na watanzania mbalimbali, kama za kweli au za uongo, ni wazi kuwa mmoja kati yao ndiye turufu ya ushindi wa kirahisi kwa CCM.

Kama siasa zingekuwa ni kufuata kigezo cha umaarufu tu na sio vinginevyo basi ni wazi kuwa wagombea wengine wangeshajitoa muda mrefu na kuupunguzia umma wa watanzania adha ya kufukiri sana kuhusu hatma ya maisha yao na nchi yao kwa ujumla. Lakini ukweli sio hivyo.

Na: Omar S Ilyas
University of Dar Es Salaam.

No comments: