KIKWETE CHAGUA MAARUFU, SALIM CHAGUO MAKINI

Published by Mtanzania Jumapili@ 2005

Hata kama kuna wengi watakaokasirika, ni ukweli ulio wazi kuwa uteuzi wa mgombea wa Urais wa Tanzania kupitia chama cha CCM utakaofanyika tarahe Mosi mwezi Mei 2005 kule DODOMA, ndio utakao amua kuwa harakati za kumtafuta rais wa Tanzania kwa miaka mitano au kumi ijayo zimekwisha au ndio kwanza zinaanza.

Nasema hivi kwa kuwa ni wazi kati ya wagombea wote waliojitokeza kuna wagombea wawili au watatu ambao wakipitishwa, sio tu watatoa nafasi kwa vyama mbalimbali vya upinzani ambavyo bado havijaweza kujiuza vyema kwa watanzania kujitutumua kisiasa na kutoa upinzani mkali kwa baba wa dola, yaani CCM.

Lakini vilevile kuna wagombea wengine wawili ambao kwa kweli CCM ikimpitisha mmoja wapo na mwingine kutopiga kelele za mizengwe, basi ushindi wa kishindo unakuwa tayari umeshajikita kwa ndugu zetu wa hawa, yaani CCM.

Wawili hao si wengine bali ni Mtanzania mmoja maarufu hapa nchini na pande zote za dunia, Dr Salim Ahmed Salim na mwengine maarufu sana hapa nchini na maeneo mbalimbali katika maziwa makuu ya afrika, Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete.

Ni ukweli usio fichika kuwa Ndugu Kikwete ni chaguo maarufu kabisa kupita wote waliojitokeza kuwania nafasi hii kupitia CCM, akifuatiwa kwa mbali ingawa hali inaonekana kubadilika kwa kasi mno, na Dr Salim Ahmed Salim.

Sababu za umaarufu huu ambao kwa kweli ni muhimu kwa taifa linalozidi kupoteza mwelekeo kila kukicha, ni nyingi na mimi nitajitahidi kuzitoa kwa kadri ya niwezavyo bila ya unafiki.

Ndugu Kikwete ambaye ni mwanasisa mkongwe ndani ya CCM tangia ujana wake, chini ya usimamizi wa Mwalimu Nyerere ambaye yeye anasahibiana naye kwa undugu wa kiapo, kwa wanaokumbuka mchango wa Sheikh Bharamiya wa kule Bagamoyo ambaye anasahibiana naye, kikwete ameweza kujitokeza kama mwnasiasa kijana tangia pale alipogombea na kushindwa nafasi hiyo mwaka 1995 akiwa na umri wa miaka 45.

Hivi sasa ndugu huyu anakaribia miaka 55, lakini kutokana na kujitambulisha zaidi na vijana ambao ndio wengi wanaonekana kumzunguka, na hulka yake ya uhalisia “simplicity”, ndugu huyu ameweza kujitengenezea mhimili wa kisiasa katika jukwaa la vijana ambao ama kwa bahati au kwa makusudi wameweza kupenyeza ngome za CCM kwa wingi kuanzia mwaka 1998 na kuendelea.

Wako wanaohoji kuwa yeye si kijana lakini ningependa kuwakumbusha kuwa ujana unaozungumziwa hapa si umri bali ni fikra, ambazo vijana walio wengi ambao ndio wamiliki halali wa taifa hili wanaamini kuwa Ndugu Kikwete pekee ndiye anayewakilisha ndoto zao za kuondokana na ufedhuli wa kimaisha unaotugubika.

Kingine ambacho Ndugu Kikwete ameweza kukiwakilisha kwa jamii, ni dhana ya uasi wa ndani UASI WA NDANI ya mfumo wa kuhafidhina wenye kuendeshwa na falsafa ya rushwa iliyokithiri ndani ya Chama kinachojiita cha Mapinduzi.

Ukiondoa karibia wote wanagombea nafasi hiyo ndani ya CCM, Ndugu Kikwete ndiye pekee mwenye kuonyesha kuwa ni kweli mwakilishi wa wakulima na wafanyakazi wa tabaka la kati na la chini kutokana na haiba yake ya uhalisia. Ndugu huyu ambaye ama kwa uthabiti wa kimaadili au mahesabu ya kisiasa, pamoja na mambo mengine ameweza kukataa “kuzawadiwa” nyumba zilizojengwa kwa jasho na damu za watanzania, kitu ambacho kinawapa matumaini vijana na wazee wengi kuwa ataweza kupambana na rushwa na hata kusafisha uozo huo ndani ya CCM na tabaka tawala kwa ujumla.

Sifa nyingine aliyonayo Ndugu Kikwete ni suala la mvuto. Hili kwa kweli ni silaha kubwa ambayo hata wenzanke wakimdhihaki vipi, kamwe hawataweza kumuangusha. Suala la sura ya mvuto ni muhimu sana kwa jamii iliyokata tama kama Tanzania.

Sio kwamba inampaa wapenzi wengi kisiasa hasa wale wa jinsia tofauti naye ambao ndio wenye kura nyingi zisizotetereka kirahisi ndani na nje ya CCM, sura na haiba ya mvuto ni silaha muhimu kwa kuongoza katika mwenendo wa siasa za kimaarufu “popular politics” ambazo wengi tunadhani zinahitajika ili kusafisha uozo wa kisiasa tulionao.

Uozo ambao umejengwa na kulindwa na baadhi ya wagombea pinzani wa ndugu huyu ambao watanzania wengi hasa vijana wangependa kuona wanatoka katika medani za kisiasa.

Sifa za Dr Salim duniani nadhani wote twazijua, sio tu kutokana na majukumu mbalimbali ya kitaifa na kimataifa ambayo aliwahi na bado amekabidhiwa na wanadunia, lakini pia haiba yake ya unadhifu wa kisiasa ya mfano wa Mwalimu wake kipenzi, hayati Mwalimu Nyerere ambayo kwa sasa imekuwa ni fimbo muhimu katika jaribio lake la kuomba dhamana ya kuwaongoza watanzania moja kwa moja kama Rais wa nchi yetu.

Mengi yamesemwa kuhusu Dr Salim lakini mimi ningependa kwa kutumia kautaalamu kangu kadogo cha uchambuzi wa siasa wanachonipatia wasomi wetu pale mlimani kwa miaka kadhaa hivi sasa, kuongezea yale machache ambayo nadhani hayasemwi au hayajasemwa bado na vyopmbo vyetu vya habari.

Kutokana na upeo wa juu alionao ndugu huyu kuhusiana na mambo ya siasa za kidunia, Wengi na hata kutoka vyama pinzani na CCM wanaona Dr Salim anaweza kuwa ndio tunu ya nchi yetu kutupeleka kwenye Demokrasia ya kweli na si kwa maneno tu bali kwa vitendo.

Kwa wengi wanovutiwa naye, hilo kwake hakuna mjadala kwani ingawa wengi hubadilika na nguvu za madaraka, kwake yeye kama aliyewahi kuwa kiongozi wa mapambano dhidi ya unyonge, ukoloni na ubaguzi wa aina yeyote popote pale duniani pamoja na kuwa mpiga mbiu mkuu wa utawala wa demokrasia ya kweli barani Afrika, kufanya tofauti utakuwa ni unafiki ambao hata mtu asiye na haiba ya aibu hataweza kufanya hilo.

Lengine ni kuwa uhusiano wake wa karibu na Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Nyerere ambye ndiye amekuwa dira yake kisisasa. Uhusiano huo na mwalimu pamoja na wale watukufu wengine wa zamani (Disgruntled old guards) ambao walilitumikia taifa kwa adabu na heshima ya juu kwa wananchi.

Hawa ni kama wazee wetu akina Judge Warioba, Mzee Ibrahim Kaduma na wengineo wachache lakini washupavu ambao hadi sasa wanajaribu kuwa nguzo na dira ya dhana ya utawala wa kamaadili ambao kwa kweli umemong’onyoka mno kama sio kuisha kabisa. Hawa wameweza kumpa Dr Salim imani ya kuwa ataweza kurudisha utawala wa nidhamu ya kimaadili nchini.

Katika safari yake kuelekea uchaguzi, Dr Salim ameweza kuonyesha kuwa mbali na kusimamia ujenzi wa uchumi imara lakini anaweza kurudisha dhana ya maadili ambayo si tu tunaihitaji kwa kulinda haka kaamani ketu kwa kulinda utu wa kila mtanzania bila ya kujali nafasi yake kiuchumi, bali pia kutupunguzi janga la ukimwi ambalo kwetu sisi ni adui kama ilivyo ugaidi wa kidini kwa Taifa la Marekani hivi sasa.

Kingine ambacho haka kaupeo kangu ka kuchambua masuala ya siasa kameweza kunionyesha ni kwa msomi kama Dr Salim ambaye sio tu wa darasani bali hata katika kufikia maamuzi yake, ni dhahiri atweza kusimamia kuona kuwa thamani ya usomi makini na wasomi wetu itarudishwa.

Katika duru ya wasomi, ingawa si wote, wengi hata wale wanaompinga kwa sababu zingine wanaamini kuwa Dr Salim ataweza kutumia vyema nafasi ya kutuongoza kunusuru hali ya mbambo katika madhabahu zetu za kisomi na elimu, ambazo sio tu hali inatisha bali pia ni hatari kubwa kwa taifa letu hasa katika dunia hii ya ushindani usiokuwa na huruma wala haiba.

Bila ya kuwa ni kiongozi anayethamini hali na mawazo wa wasomi, kutambua umuhimu wa ELIMU BORA na sio BORA ELIMU, anayejiongoza kisiasa na kuwaongoza wananchi wake kwa lugha na mtindo wa kisomi, ni wazi hata tukiletewa malaika, safari ya tunapoelekea kusikojulikana itakuwa ya mwendo kasi na wa hatari mno.

Lingine ambalo kwa kweli si ajabu kuona watanzania wengi wa kizazi chetu hawakioni ni kuwa watanzania kama washika dau wakuu wa dunia ya tatu, au kwa kifupi masikini wa dunia, hivi sasa tunakabiliwa na zoezi kubwa la kupambana kuweza kupata mfumo wa siasa za kimataifa ambo utatambua na kutetea zaidi maisha yetu kiuchumi na kijamii kwa miaka mingi ijayo.

Hili ni suala la marekebisho mbalimbali katika mfumo wa umoja wa mataifa (UN) ambao kutokana na mchango wa Dr Salim na viongozi wenzake wengi wapatao kumi na tano pamoja na wasomi wetu kama Prof Mwesiga Baregu na Prof Haroub Othman, kuanzia mwezi September 2005 kule New York, Marekani na kwengine pote duniani, majadiliano makali yataendelea kujaribu kubadili mfumo wa kimataifa.

Mfumo ambao kwa miaka mingi umekuwa ukiwapendelea mno mataifa makubwa na tajiri dunia na kukandamiza ndoto zetu za kupata ahuani ya kweli ya kimaisha. Kwa kweli kama hatutakuwa na kiongozi shupavu, makini, msomi, mwenye kuheshimika katika medani za kimataifa na mjuzi wa hali ya juu wa masuala haya, Tanzania ambayo ina jukumu la kuongoza sauti ya wanyonge kupitia nafasi yetu katika baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kama mwanachama wa muda kwa miaka miwili kuanzia mwezi January mwaka huu, ni dhahiri mpambano huu tunaweza tukaupoteza hivyo tukawa tumejisaliti na kuwasaliti mabilioni ya wanadunia masikini na wanyonge wanaotegemea sauti yetu huko.

Nasisitiza hili kwa sababu najua wazi kuwa bila ya kubadili mfumo wa siasa wa kimataifa, hata kama utaletewa malaika wa juu kabisa, kamwe mbio zetu zitaishia ukingoni na kuendelea na siasa za longolongo, kama wanavyosema vijana wa mjini.

Ukiangalia hizo baadhi ya sifa za wagombea hawa wawili wa CCM hapo juu na nyingine nyingi zilisosemwa na zinazosemwa na watanzania mbalimbali, kama za kweli au za uongo, ni wazi kuwa mmoja kati yao ndiye turufu ya ushindi wa kirahisi kwa CCM.

Kama siasa zingekuwa ni kufuata kigezo cha umaarufu tu na sio vinginevyo basi ni wazi kuwa wagombea wengine wangeshajitoa muda mrefu na kuupunguzia umma wa watanzania adha ya kufukiri sana kuhusu hatma ya maisha yao na nchi yao kwa ujumla. Lakini ukweli sio hivyo.



SEHEMU YA PILI: CCM inavuna ilichopanda..........

Wiki iliyopita nilijaribu kuwaelezea wagombea wawili na kwa nini wameweza kuonekna kwa upeo wa wengi kuwazidi wenzao wengine katika nafasi ya umaarufu sio tu ndani ya CCM bali kwa watanzania kwa ujumla. Leo napenda kuendelea uchambuzi wangu kwa kuongelea siasa za uchaguzi kwa ujumla kama zinavyoendelea.

Tofauti na wenzetu katika demokrasia zilizoendelea kule ughaibuni yaani sehemu kubwa ya Ulaya na Amerika kaskazini, Watanzania na Tanzania kama nchi na dola lake wana vigezo tofauti kidogo katika kumchagua kiongozi wa aina yoyote ile katika medani ya kisiasa. Kama ingekuwa ni suala la uzoefu na mvuto tu ndio turufu pekee basi kama nilivyosema wakati ule, mbio za uchaguzi zingekuwa zimekwisha. Lakini kwa jinsi ninayoona mimi, siasa za uchaguzi za CCM na Tanzania kwa ujumla kwa wakati huu zimejitwika katika maeneo kadhaa yafuatayo.

Moja kubwa ni nafasi ya matakwa binafsi ya mtanzania mmoja mmoja bila ya kujali maslahi ya taifa kwa ujumla, ukiachilia bara la afrika na dunia yetu. Hili limejitokeza sana katika mijadala mbalimbali inayoendelea katika kila pande ya nchi yetu. Suala la mimi nitafaidka na nini kutoka kwa nani ndilo haswa limejikita kati ya wapiga kura wa CCM katika vikao vikuu vya chama ambavyo ndivyo vitateua mwakilishi wao katika kugombea nafasi ya Urais hapo Oktoba.

Suala hili ambalo kwa kiasi kikubwa limechangia kuweko kwa uchambuzi unaolenga zaidi majina ya wagombea na sio vigezo vya wagombea bora ndilo pia limekuwa dira ya uchaguzi miongoni mwa watanzania wa ngazi na kada zote nchini, kuanzia wafanyabiashara wa aina zote, kubwa na ndogo, halali na haramu, wasomi, wafanyakazi na wasio na kazi, wakulima na wafugaji, na zaidi waandishi wa habari wetu.

Wengi wetu tumegubikwa na kuangalia upatikanaji wa kirahisi wa mahitaji yetu binafsi ya muda mchache na kusahau au kutotilia umuhimu mahitaji ya muda mrefu ya taifa letu tukufu. Hili limetufanya tuongelee siasa kwa msingi wa majina zaidi ya uwezo na vipaji vya wenye majina hayo kwani kwetu bora ni yule tunayemuona tunashabihiana naye kama ni kidini, kikabila, kirika, kifikira, kijamii, kiuchumi na hata kirangi!!!.

Hata hivyo itakuwa ni dhambi kubwa kwa kuwalaumu watanzania kwa kosa hili, yaani kutumia maslahi binafsi kama ndio dira pekee ambayo watanzania tulio wengi tunaitumia kuamua nani anafaa na nani hafai. Dira hii potofu ya uchaguzi iliyotanda katika fikra za watanzania walio wengi, sio tu inatawala katika suala zima la kuchagua rais kwa sasa lakini pia hata katika masuala mengine yoyote ya kimaisha iwe rafiki, thamani za nyumba, kazi, aina ya elimu, na memnngineyo mengi kma sio yote.

Dira hii ambayo imepandwa na kupaliliwa na dhana ya kihafidhina inayoendeshwa na falsafa ya unyang’au yenye kupitia njia ya BORA ELIMU, ambayo ndiyo iliyozaa taifa lenye upungufu wa umakini, tupende tusipende ina nafasi kubwa ya kuiamulia CCM nani anakuwa mgombea wao na si nani mgombea bora kutoka kwao.

Tafiti mbali mbali zimefanywa na wasomi wetu na zimeonyesha wazi kuwa watanzania kwa kiasi kikubwa wamepunguza umakini wao katika kuchagua kinachowafaa na hivyo kujiweka VULNERABLE na siasa za kiujanja ujanja ambazo zina mvuto wa faida au mapato ya kirahisi rahisi na sio yenye umakini wa kutufaidisha kwa muda mrefu.

Hili linatokana na sera ya BORA ELIMU inayoendeshwa na wakubwa hawa kwa muda mrefu sasa ambayo inalenga kupata watanzania wa aina ya ndiyo mzee na sio wakorofi wenye chachu ya kuhoji. Sera ambayo umuhimu wake mkubwa umetokana na kuporomoka kwa uwezo wa kiutawala wenye kuamini maadili ya uongozi na umakini wa kiuongozi kitu ambacho kimefuatana kwa pamoja na mfumuko wa madhila ya kimaisha ambao umepelekea kumomonyoka kwa uhalali wa kisiasa wa tabaka tawala la nchi yetu.

Ninasema kuwa CCM inavuna ilichopanda kutokana na hali inayojionyesha hivi sasa ya kuwa njia panda iliyojikuta imewekwa na kampeni za baadhi ya wagombea wake. Hali ambayo imewaweka katika hatari ya kupata bora mgombea atakeyewahakikishia ushindi wa kishindo na sio mgombea bora ambaye sio tu atahakikisha kujenga nyufa zinazojitokeza ndani ya muhimili ya chama na dola bali pia atarudisha sifa ya chama hiki kinachoelekea kaburini kwa mwendo wa mwanga wa taa. Mtu ambaye kutokna na haiba, upeo na mtazao wa kimaadili atweza kukirudishia chama hiki sifa iliyopotea ya kuwa ni chama imara, chenye nidhamu na kinachiaminika kama kimbilio la wengi na wananchi.

Ukifuatilia kwa ndani sana mwenendo wa siasa ndani ya chama hicho hasa matamshi ya viongozi wa juu wa chama hicho, ni dhahiri kuwa kama jadi yake tangia enzi za Baba wa Taifa, hayati mwalimu Nyerere, tayari watukufu wachache wamekwishaamua nani anakuwa mrithi wa rais Benjamin Mkapa.

Hata kama manung’uniko ni mengi miongoni mwao lakini ni wazi hali ya kampeni zinazoendelea zimewapelekea kuamua kuchukua uamuzi mzito mno miongoni mwao wa kuhakikisha chama kinatoa mgombea makini ambaye sio tu kwa uzoefu wake na haiba ya yake ya umakini ataweza kupambana na uasi wa watanzania kama watakosea kuchagua, lakini pia uasi ndani ya chama ambao ndio tishio kubwa zaidi kuliko mengine.

Lakini kwa jinsi hali ilivyo, ingawa kuna mabadiliko ya upepo wa kisiasa unaotokea kwa kasi kubwa ambayo haikutegemewa na walio wengi, kazi ya kuwabadilisha mawazo watanzania walio wengi na hasa wapiga kura wa CCM inakua ngumu mno kama si ya hatari sana.

Ni wazi wengi wao wameshaweka msimamo wao, na utmaduni wa mtanzania kwa kweli ni wa kutokuwa tayari kufanya mabadiliko makubwa ya kimaamuzi kwa urahisi (conservatism) hivyo majaribio haya ambayo ukiyatazama kwa undani ni yenye nia njema kabisa ya kuwahakikishia wana CCM na na hasa watanzania kwa ujumla, kuwa chaguo litakaloletwa na CCM ambao wao (watukufu wachache) tayari wamelikubali ndilo bora zaidi na makini kwa CCM na watanzania kwa ujumla, limekumbwa na ugumu wa kipekee kabisa.

Ugumu huu unatokana na kuwa chaguo hilo sio lile ambalo wengi wamekwisha amua kuwa ndio la manufaa yao na hivyo kudhani kuwa ndio la manufaa ya taifa. Vilevile dhana ya uwezekano wa uasi wa kiasiasa wa wananchi na wana CCM walio wengi kwa ujumla wakiwemo nuru ya tamaa ya mabadiliko kwa walio wengi, yaani baadhi ya wagombea vigogo, inawafanya watukufu hawa ndani ya medani za juu za CCM kuwa na mtihani mzito mno.

Kwa ujumla ugumu huu chanzo chake kikuu kinatokea katika aina ya usomi wa watanzania walio wengi ambao umewapelekea kuamini mengi bila ya uchambuzi wa kina na wa makini hivyo kiurahisi kabisa kuamua nani atakayewatatulia madhila yao kwa wale waliogubikwa nayo na kuwaongezea zaidi wale walifaonikiwa kwa kiasi, ambao wangependa kufika juu zaidi na kuwapiku wale waliojisimika huko kwa muda mrefu mno.

Kama watukufu hawa wangeona kuna umuhimu wa kuendeleza ELIMU BORA yenye kugubikwa na dhana na fikira za uzalendo wa kweli wenye kuneemeshwa na chachu ya kuhoji, basi kazi ya kuwashawishi wana CCM na watanzania walio wengi kuwa chagua wanalowapa ndilo bora zaidi kwao na kwa Tanzania kwa ujumla sio tu kwa wakati huu bali hata kwa wakati ujao, isingekuwa ngumu na ya hatari kama inavyonekana hivi sasa.

Kazi nyengine ambayo ndiyo kubwa zaidi inayowagubika wakuu hawa wa CCM ni kupambana na upinzani mkali utakaotoka kwa wapambe wa mgombea maarufu ambaye inaonyesha tayari wameshamuona kuwa ni hatari kwa maslahi ya nchi kama waonavyo wao ingawa wanakubali kuwa ndio mgombea maarufu kuliko wote.

Wapambe hawa ambao wengi wana upeo wa hali ya juu wa propaganda za kisiasa wakisaidiwa na nafasi ya kukubalika kwao ingawa sio wote katika jukwaa la vijana walio wengi ambao ndio nguzo ya umaarufu wa CCM, ni dhahiri hawatakuwa tayari kuona kuwa wanapokonywa nafasi ya wao pia kupenya na kuchukua nafasi za juu kisiasa nchini kutoka kwa wanasiasa wakongwe au wazee kwa lugha maarufu hivi sasa.

Hata kama mgombea wao waliyeweza kumhakikishia umaarufu wake kwa wananchi walio wengi mno kwa utaalamu wa hali ya juu wa kipropaganda halali na haramu, atakubali yaishe ile naye ajihakikishie kuendelea kwa nafasi na umuhimu wake kisiasa kwa gharama nafuu, ni wazi wapambe hawa wanajua wazi kuwa ndoto zao nyingi hazitafanikiwa na pengine hata wakapoteza umuhimu wa kisiasa na kijamii wanaotmba nao hivi sasa.

Hofu hii inaonekana wazi hivi sasa kiasi ya kuwa wale wachache ambao wanasukumwa na uzalendo wao kwa nchi zaidi ya mafanikio yao binafsi wameshaanza kuona umuhimu wa kujenga daraja kati yao na mgombea makini ambaye kwa njia moja au nyingine ndiye kimbilio lao.

Lakini hili nalo linaweza kuwa tatizo kwa watukufu wa CCM wanaojaribu kuhalalisha uamuzi wao wa kumrithisha mgombea wanayemuona ni makini na bora zaidi kwa chamaa kwanza na jamii kwa ujumla.

Ni tatizo kutokana na kuwa endapo daraja hili litajengeka vema na mgombea maarufu ambaye hadi sasa ana uhakika mkubwa wa kushinda kinyang’anyiro hicho endapo hakutakuwa na kile wengi wanakiita mizengwe na wasomi wanaita ukweli wa kisiasa, na akakubali yaishe mapema. Ni wazi kuwa kundi lengine la wagombea ndani ya CCM halitakubali kushindwa kirahisi.

Kundi hilo linawahusisha wagombea wengine wawili au watatu ambao kwa hali ilivyo linaweza kuondoa uwezekano wa kumaliza uchaguzi mwezi Mei na kufanya uendelee hadi Oktoba na pengine zaidi ya hapo kutokana na uwezekano mkubwa wa kuamsha upinzani wa hali ya juu kutoka kwa watanzania walio wengi ambao wamejengewa dhana ya kuwa hao ni maadui wa amani na maendeleo yao.

Kundi hili linaweza kuleta madhara makubwa kwa CCM na watanzania wote kwa ujumla, kutokana na ukweli ulio wazi kuwa muungano au makubaliano yoyote kati ya MGOMBEA MAARUFU na MGOMBEA MAKINI unaweza au yanaweza kuwahakikishia wengi wao mwisho wao kisiasa, kitu ambacho kwa siasa za dunia yetu ya tatu kama ilnavyojionyesha kwa majirani zetu, maana yake inaweza hata ikawa mwiso wao kimaisha.

Kundi hili litajaribu kutumia kila aina ya mbinu, halali na haramu kujaribu kuzuia hali hiyo, kitu ambacho kitaendeleza mpasuko ndani ya CCM na mbaya zaidi kwenye vyombo muhimu na nyeti vya dola ambavyo ndivyo kwa miaka mingi sasa vimekuwa mihimili muhimu kwa tabaka tawala na taifa kwa ujumla.

Wapo wanaofikiri kuwa mpasuko ndani ya CCM utakuwa neema kwa watanzania kwani utawezesha wananchi walio wengi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitafuta chama mbadala na kushindwa kukiona nje CCM, kuamini kuwa upinzania unaweza kuwa nusura yao.

Dhana hii ina ukweli wake lakini kwa bahati mbaya kwa jinsi mambo yanavyokwenda, kuvunjika kwa CCM kwa staili inayojionyesha ni wazi kutafuatana na kuvunjika kwa dola hivyo kusababisha hasara kubwa kwa Taifa kwa ujumla.

Hii inatoka ukweli kuwa tofauti na katika nchi za wenzetu kama Kenya na kwengineko, hapa kwetu CCM si chama tawala tu bali ni chama dola. Pale inapotokea kinavunjika kwa siasa za chuki na visasi kama tunazoziona sasa ni dhahiri viongozi wa juu wa CCM hawataweza kuhakikisha usalama wa dola ambalo kwa bahati mbaya limeachana na wajibu wake wa kuwa msimamizi wa siasa ndani ya chama tawala na kuwa sehemu ya ushindani wa kisiasa ndani ya mpambano huu.

Suala hili la hatari ya kuvunjika kwa dola ndilo haswa limepelekea sio tuu viongozi wa kisiasa makini wa nchi yetu pamoja na viongozi wa kidini na kielimu kujawa na woga wa hali juu na kujikukuta wako njia panda katika kutimiza wajibu wao wa kulinda tabaka tawala na hivyo jamii kwa ujumla.

Hii inatokana na ukweli kuwa ni wazi hata kama mambo yakawa shwari hata baada ya CCM kuchagua yeyote yule wanayempenda na wanaona anawafaa, kuna hatari kubwa kuwa mara baada ya mmoja wa hawa wanaochuana kwa nguvu zote atakapokabidhiwa dhamana ya ulinzi na usalama wa taifa wa nchi yetu, itambidi kuchukua hatua za kusafisha chama na dola na kuondokana na vile vinasaba vilivyokuwa vikimpinga waziwazi alipokuwa anawania kuteuliwa na chama au hata wakati wa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba.

Hilo halitakuja tu kwa ajili ya chaguo maarufu kujihakikishia usalama wake bali pia litambidi kufanya hivyo kwa ajili kujaribu kukidhi hamu kubwa ya wafuasi wake waliompigia debe na kumshindisha kwa kishindo. Hamu ambayo imejengwa katika dhana ya usafi wa kisiasa na uthabiti wa ki hulka ambao wengi weu tunadhani ni silaha muhimu katika kuondoa unyang’au huu unaotukumba hat kama kuna hatari gani itayoukumba hapo mbeleni. Wanasayansi wa kisiasa kuchambua dhana hii kama mwisho unahalalalisha njia (ends justifies the means).

Na endapo atapita mtu anayetoka kwenye upande ule mwingine, yaani wale ambao CCM inaona watakuwa mzigo mzito ku-ubeba lakini kutokana na nguvu mbalimbali zikiwemo za dola na udhaifu wa baadhi ya viongozi wa vyama kadhaa pinzani wa CCM, wanaweza kushinda mwezi Oktoba, ni wazi itabidi wajikoshe kwa watanzania ili kujihalalishia nafasi zao.

Hapa pia kuna hatari ya kuwaona kina Mutharika wengine ambao ingawa wao wenyewe ni wachafu wa kutupwa lakini wangependa kuwabebesha wengine lawama ili wao waonekane ni malaika. Hili lazima litaleta vurugu zaidi miongoni mwa tabaka tawala na kuathiri uthabiti wa mhimili wa amani yetu yaani dola.

Kwa hali hiyo hapo juu na sababu nyingine kadhaa wa kadhaa, ni wazi CCM kwa sasa inavuna ilichopanda kwa kujikuta njia panda baada ya kushindwa kwa viongozi wa juu ambao daima ndio wamekuwa watoa uamuzi wa kweli wa nani anamrithi nani, kusimama wazi na kuwaonyesha wana CCM na watanzania kwa ujumla chaguo wanaloliona wao kuwa makini na bora zaidi dhidi ya chaguo maarufu zaidi, na wangependa wananchi kupitia watukufu wachache kule DODOMA kuridhia chagua hilo kwa kile waonavyo wao nap engine kuna ukweli, ni kwa manufaa ya taifa.

Hii ilikuwa ni makala maalumu wakati tunaelekea kule Chimwaga mwaka 2005..

No comments: